Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 18:56

Kutoweka kwa mpinzani Eugene Ndereyimana na wengine nchini Rwanda


Rais Paul Kagame
Rais Paul Kagame

Wakati Eugene Ndereyimana alipoamka asubuhi wiki iliyopita, hakumwambia mkewe kule alikokuwa anakwenda, na mkewe hakumuuliza. Kidogo alichokuwa anajua mkewe, alifikiri ilikuwa ni bora kwake.

Baba wa watoto wawili mwenye umri wa miaka 29 alikuwa anafanya safari kutoka nyumbani kwake huko kusini mashariki ya Rwanda, Wilaya ya Ngoma kuelekea magharibi mashariki mji wa Nyagatare kwa ajili ya mkutano wa kisiasa Julai 15.

Lakini watu waliokuwa wanamsubiri Ndereyimana kuwasili kwenye mkutano walipoteza mawasiliano naye baada ya kuwa amefika kilomita tano (maili 3.1) kufikia sehemu inayofanyika mkutano. Tangu wakati huo hajaonekana wala kuwa na mawasiliano na mtu yoyote.

Eugene Ndereyimana alitoweka wiki iliyopita

Ndereyimana ni mwakilishi wa chama cha FDU- Inkingi, muungano wa vyama vya upinzani vinavyompinga Rais Paul Kagame ambavyo havijasaliwa. Rais Kagame amekuwa madarakani tangu mwaka 2000.

Ndereyimana ni mmoja wa wanachama wasiopungua watano ambao wametoweka katika mazingira yasiyojulikana kwa kipindi cha miaka michache iliyopita chini ya utawala wa Kagame, Rwanda.

Wanasiasa wa upinzani na wanachama wanaounga muungano wa siasa huo mkono wanasema wanakabiliwa na vitisho, uvunjifu wa amani, vifungo au uwezekano wa kutoweka kwa kutekwa pale wanapoonyesha upinzani dhidi ya Rais na chama chake tawala, Rwandan Patriotic Front (RPF).

Hata hivyo Kituo cha Habari cha CNN ambacho kimeripoti taarifa hizi kimeeleza juhudi za kupata majibu juu ya tuhuma hizi kutoka ofisi ya Rais na Chama cha RPF hazikufanikiwa kwa kuwa hawakutoa majibu.

Kwa upande wa Ndereyimana vitisho vilianza dhidi yake mwezi Septemba mwaka 2018, wakati alipowekwa kizuizini kiholela na maafisa wa jeshi katika kituo cha eneo cha polisi, mkewe Joseline Mwiseneza ameiambia CNN, kupitia kwa msemaji wa upinzani.

“Kwa upande wao (serikali) yeye ni adui,” Mwiseneza amesema, akiwa anaelezea serikali za mitaa. Ameongeza kuwa shughuli za kisiasa anazofanya Ndereyimana zimemsababishia matatizo katika maisha yake ya kila siku – ikiwemo kubughudhiwa na vyombo vya usalama mpaka kunyimwa mikopo kutoka katika benki za kieneo.

Ofisi ya uchunguzi ya Rwanda na Jeshi la Polisi la Rwanda hawakujibu chochote pale CNN ilipotaka watoe maelezo.

Hivi sasa, Mwiseneza anasema kuwa hajui awaambie nini watoto wake, ambao wanaendelea kumuuliza pale alipo baba yao, na anahofia maisha ya mumewe.

Wakati akingojea majibu, wanasiasa wengine walioko pamoja naye wamekabiliwa na vitendo vya uvunjifu wa amani.

Kuuawa kwa Anselme Mutuyimana

Katika kesi ya kuhuzunisha mwezi Machi, Anselme Mutuyimana mwenye umri wa miaka 30, msaidizi wa karibu wa rais wa FDU Victoire Ingabire, alikutwa amekufa msituni katika mkoa wa kaskazini magharibi ya nchi hiyo.

Wakazi waliouokata mwili wa Mutuyimana walisema inavyoelekea alikufa kwa kunyongwa, kwa mujibu wa chama chake.

Wakati huo, Ofisi ya Upelelezi ya Rwanda iliiambia CNN kuwa uchunguzi umeanza juu ya mauaji yake na hakuna mshukiwa yoyote aliyekamatwa.

Katika tukio jingine Octoba 2018, mfungwa ambaye ni Makamu Rais wa Chama cha FDU Boniface Twagirimana alitoweka kutoka katika gereza lenye ulinzi mkali ambako alikuwa akishikiliwa kwa siku tano baada ya kuhamishwa kutoka gereza jingine.

Wachama wa nane wa FDU

Twagirimana na wanachama wengine nane wa chama cha FDU walikuwa wanatumikia kifungo baada ya kukamatwa mwaka 2017 kwa tuhuma za kuunda vikundi vyenye silaha na kutaka kuipindua serikali ya Kagame, mashtaka ambayo Twagirimana ameyakanusha.

Pale kiongozi huyo alipotoweka, Viongozi wa Gereza hilo lenye ulinzi mkali walisema kuwa alikuwa ametoroka. Maafisa wa chama cha FDU wanasema kuwa hizo ni “mbinu za uovu.”

Wakizungumzia kesi ya Twagirimana mwezi Novemba, shirika linalofuatilia haki za binadamu Human Rights Watch (HRW) limesisitiza kuwa “kupotezwa kwa watu hao siyo kitu kigeni” nchini Rwanda. HRW inasema imeweza kukusanya ushahidi juu ya juhudi za serikali zinazoendelea kunyamazisha wanaoikosoa na wale wanaoonekana ni wanasiasa wapinzani (wa Kagame) katika miaka ya karibuni kwa ukamataji holela, vitisho, na kutoweka kwa watu hao.

XS
SM
MD
LG