Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 13:46

Baada ya madai ya udukuzi AU, Huawei zaimarisha ushirikiano


Mwenyekiti wa Tume ya AU Moussa Faki
Mwenyekiti wa Tume ya AU Moussa Faki

Viongozi wa Umoja wa Afrika (AU) wameamua kuimarisha mahusiano kati yake na kampuni ya teknolojia ya China wakati ambapo ukosoaji wa kimataifa umeongezeka dhidi ya kampuni hiyo.

Wakati tuhuma za ujasusi dhidi ya China zilipojitokeza mwanzoni mwa mwaka 2018, Moussa Faki, mwenyekiti wa Tume ya AU, na Hailemariam Desalegn, waziri mkuu wa zamani wa Ethiopia, walikanusha tuhuma hizo, kama ilivyokuwa kwa maafisa wa China.

Kampuni ya Huawei ilizitaja tuhuma hizo “hazina ushahidi wowote” na kusema wao kwa “nguvu zote wanakanusha” madai yoyote ya uchochezi.

Ni aina gani ya taarifa ambayo ilikuwa imedukuliwa, na kwa nini serikali ya China ione kuwa taarifa hiyo inathamani, ni jambo ambalo bado linatatanisha.

Lakini tuhuma hizo zinaendana na aina ya ukosoaji mpana zaidi dhidi ya Huawei.

Mwaka 2012, Kamati ya Usalama ya Baraza la Wawakilishi la Marekani iliiainisha Huawei kuwa ni tishio kwa usalama wa taifa na kuonya kuwa imeiba haki miliki na huenda ikawa inafanya ujasusi dhidi ya Wamarekani kwa “kufanya udukuzi” unaoiwezesha kupata takwimu muhimu za siri ambazo hawaruhusiwa kuzijua.

Shinikizo dhidi ya kampuni hiyo ziliongezeka mwezi uliopita, wakati Idara ya Biashara ya Marekani ilipoiweka Huawei katika “orodha ya makampuni,” yaliyowekewa vikwazo vya biashara na washirika wa Marekani, baada ya Rais Donald Trump kutoa amri ya kiutendaji mara moja inayozuia kampuni hiyo kuendesha shughuli zake nchini Marekani.

Wakati ukosoaji huo ukiendelea kuongezeka duniani, Huawei ilithibitisha uwepo wake wiki iliyopita wakati iliposaini mkataba na Umoja wa Afrika kuongeza ushirikiano katika idadi kadhaa za teknolojia, kuanzia teknolojia ya masafa marefu na “Cloud”( inayotumika kufikia mitandao ya seva zilizo mbali zinapatikana katika Intaneti kuhifadhi, kusimamia na kutayarisha takwimu nje ya kompyuta unayotumia) na mawasiliano ya teknolojia ya 5G na matumizi ya mifumo inayoigiza kile ambacho kinafanywa na mwanadamu.

Thomas Kwesi Quartey, naibu mwenyekiti wa Tume ya AU na Philippe Wang, makamu wa rais wa Huawei Afrika Kaskazini, walisaini mkataba wa makubaliano wiki iliyopita katika makao makuu ya AU – ikiwa ni hatua ya zawadi ya urafiki kutoka China kwa ajili ya Afrika – huko Addis Ababa, Ethiopia.

Mkataba huo ni kuonyesha umoja wakati huu mgumu katika historia ya Huawei – na uwezekano wa kuhitalafiana Afrika na Marekani wakati huu ambapo uhasama kati ya nchi zenye uchumi mkubwa kuliko zote ukiongezeka.

Pia inaongeza uwepo wa Huawei katika soko pakiwepo uwezekano mkubwa wa kukua kwa kampuni hiyo miaka inayokuja – wakati asilimia 36 tu ya Waafrika wakiwa na huduma ya kuaminika ya intaneti hadi Machi 2019.

Huawei mara ya kwanza iliingia katika soko la Afrika mwisho wa mwaka 1990, wakati iliposaidia kujenga mitandao ya simu za mkononi katika darzeni ya nchi mbalimbali – wataalamu wanakadiria kuwa Huawei ilijenga idadi kubwa ya miundombinu ya simu za mkononi za Afrika, na kuleta athari chanya katika sekta mbalimbali katika safari yake hiyo, kuanzia nyanja ya elimu na benki mpaka afya na serikali.

Mitandao ya mawasiliano iliyojengwa na Huawei, kupitia mikopo inayofadhiliwa na serikali ya China, haijulikani sana kama vile miradi mikubwa ya miundombinu mingine kama vile madaraja na reli. Lakini athari ya miradi hiyo bado imewafikia watu wengi.

XS
SM
MD
LG