Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 02:07

Rais wa Marekani apiga marufuku matumizi ya vifaa vya kampuni ya Huawei


Maafisa wa Marekani wameanza kutekeleza marufuku inayokataza kampuni ya simu ya China, Titan Huawei kutengeneza simu ya mkononi aina ya mtandao wa “5G” nchini Marekani na wanatahadharisha kuwa kampuni hiyo ina hatarisha usalama wa nchi nyingine.

Jumatano, Rais wa Marekani Donald Trump amesaini amri ya kiutendaji inayokataza kampuni za Marekani kutumia kifaa cha mawasiliano kinachotengenezwa na makampuni ambayo yanahatarisha usalama wa taifa. Amri hiyo, ambayo imetangaza hali ya dharura ya kitaifa, ni hatua ya kwanza ya kurasimisha katazo hilo la kufanya biashara na kampuni ya Huawei.

Kwa upande wake, hata hivyo, Huawei imeonyesha haina dalili yoyote ya kurudi nyuma, na imekuwa ikitoa ahadi zisizokuwa za kawaida ili kuweza kuwashinda wakosoaji wake na kukanusha madai ya kuwepo tishio la usalama. Kampuni hiyo inasema itasitisha biashara iwapo itashinikizwa kufanya ujasusi dhidi ya wateja wake na hivi sasa mwenyekiti wa kampuni hiyo Liang Hua amependekeza kusaini mikataba ya "kutojihusisha na ujasusi.”

Akizungumza kupitia mkalimani wakati wa ziara yake London, Liang amesema kuwa Huawei iko tayari “ kuchukua ahadi kufanya vifaa vyetu vifikie viwango vya kutokuwepo ujasusi, na udukuzi wa siri.”

Haikufahamika kile Liang alichokuwa anakusudia kwa kusema “hakuna ujasusi, wala udukuzi wa siri", ilivyokuwa Huawei kama makampuni mengine ya teknolojia inawataka wateja wake kusaini makubaliano ya kuruhusu uwezekano wa kampuni hiyo kushirikisha serikali za eneo kutumia taarifa binafsi za wateja iwapo watazihitaji.
Kampuni nyingi za teknolojia, kama vile Google na Facebook huwa zinatoa taarifa zinazohitajika na serikali katika ripoti za kawaida za umma. Kampuni hizo zinatoa maelezo pale zinapokuwa zimeridhia kutekeleza maombi ya serikali na wakati wanapowapinga mahakamani.

Hakuna taarifa juu ya aina gani ya takwimu ambazo Huawei inatoa kuzipa vyombo vya usalama vya Beijing. Iwapo maafisa wa China ndio wanaoamua yale yanayohusika “siri za nchi” au uchunguzi wa jinai, maafisa wanaweza kuhalalisha kudukua aina yoyote ya mawasiliano. Wakosoaji wanasema Beijing inaeleza “Siri za nchi” kiholela na inaweza kuhusisha takriban kila kitu.

Katika maoni yake kwa waandishi, Liang amesema Huawei hafanyi shughuli zake kwa niaba ya serikali ya China katika soko lolote la kimataifa.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Uingereza Reuters, alikanusha kuwa sheria za China zinazitaka kampuni “kukusanya taarifa za siri za nchi nyingine kwa ajili ya serikali au kutengeneza vifaa vya udukuzi wa siri hizo kwa ajili yao.”

Ameongeza kusema kuwa Huawei imejizatiti kufuata sheria na kanuni za kila nchi ambako inafanya biashara.

XS
SM
MD
LG