Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 13:14

Mvutano wa Kibiashara : Trump kukutana Alhamisi na makamu Waziri Mkuu wa China


Makamu Waziri Mkuu wa China Liu He, kati, na ujumbe wake wakihudhuria mkutano wa kibiashara Washington.
Makamu Waziri Mkuu wa China Liu He, kati, na ujumbe wake wakihudhuria mkutano wa kibiashara Washington.

Rais wa Marekani Donald Trump atakutana na makamu Waziri Mkuu wa China Liu He White House Alhamisi, ikiwa ni siku ya mwisho ya duru ya pili ya mazungumzo yanayo kusudia kutafuta ufumbuzi wa mvutano wa kibiashara unaoendelea kati ya mafahali wawili wa kiuchumi duniani.

Liu He, mzungumzaji mkuu wa masuala ya biashara ya China, alikutana Jumatano na wajumbe wa Marekani wanao ongozwa na Mwakilishi wa Biashara Robert Lighthizer kwenye jengo la ofisi ya utendaji iliyoko pembezoni ya White House.

Ujumbe huo uliendelea na mazungumzo juu ya malalamiko ya muda mrefu ya Washington kuwa Beijing inayalazimisha makampuni ya Marekani kuhamisha teknolojia yao ya kiwango cha juu kwa makampuni ya China na kuzuia kampuni hizo kuingia katika soko pana la China.

Mazungumzo hayo yalihofiwa kuwa yangegubikwa na hatua ya waendesha mashtaka ya kumkuta na kosa la kujibu Meng Wanzhou, afisa mkuu wa uhasibu wa kampuni kubwa ya teknolojia ya mawasiliano ya Huawei ya China.

Tuhuma hizo anazotakiwa kuzijibu afisa huyo zinadai kuwa Meng, Huawei na washirika wake walikula njama kukiuka vikwazo vilivyo wekwa na Marekani dhidi ya Iran na kuzidanganya taasisi za fedha na serikali ya Marekani juu ya shughuli zao.

China ilikasirishwa na kitendo cha Meng kukamatwa huko jijini Vancouver na vyombo vya usalama vya Canada Disemba 1 kwa ajili ya kupelekwa Marekani kujibu mashtaka.

Mazungumzo hayo yanatokana na makubaliano ya mwezi Disemba kati ya Rais Trump na Rais wa China Xi Jinping kuacha kulipiziana kisasi, katika mzozo juu ya utozaji ushuru kati ya nchi hizo mbili, kwa siku 90 kuanzia siku ya mwaka mpya 2019.

Uongozi wa Trump uliiadhibu China kwa kuweka ushuru juu ya bidhaa zake zinazo ingizwa Marekani zenye thamani ya dola bilioni 250 kuilazimisha China kubadilisha mwenendo wake wa kibiashara, kitu kilicho sababisha Beijing kulipiza kisasi kwa kuongeza ushuru wa bidhaa zinazo safirishwa na Marekani kwenda China zenye thamani ya dola bilioni 110.

IIwapo makubaliano hayatafikiwa ifikapo Machi 2, ushuru ulioanzishwa na Marekani utaongezeka kutoka asilimia 10 hadi 25.

XS
SM
MD
LG