Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 21:55

UN kusikiliza mgogoro wa Israeli na Wapalestina


Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu (kushoto), Rais wa Palestina Mahmoud Abbas,
Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu (kushoto), Rais wa Palestina Mahmoud Abbas,

Viongozi wa nchi mbalimbali duniani wanaoshiriki katika mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa jijini New York wanatarajiwa Alhamisi kusikiliza yanayojiri katika mgogoro wa Israeli na Wapalestina wakati maafisa kutoka pande hizo mbili watapopatiwa nafasi ya kuhutubia mkutano huo wa kila mwaka.

Rais wa Palestina Mahmoud Abbas amepangiwa kutoa hotuba yake asubuhi. Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu yuko Israeli akijaribu kuunda serikali baada ya uchaguzi uliofanyika wiki iliyopita, na hivyo Waziri wa Mambo ya Nje Israel Katz atahutubia Umoja wa Mataifa mchana kwa niaba yake.

Hali ya utata inayoendelea kuhusu kujitoa Uingereza Umoja wa Ulaya inawezekana ikawa katika ajenda huku Rais wa Baraza la EU Donald Tusk akiwa amepangiwa kutoa hotuba yake.

Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson hakuzungumza juu ya Uingereza kujitoa EU – Brexit katika hotuba yake wiki hii, na amepata kipigo kutokana na uamuzi uliyotolewa na Mahakama ya JUU ya Uingereza ikisema uamuzi wake wa kusitisha shughuli za bunge ulikuwa kinyume cha sheria.

Siku ya Jumatano huko UN Rais wa Iran Hassan Rouhani alihutubia akiwaeleza viongozi mbalimbali wa dunia kuwa hakutakuwa na mazungumzo baina ya nchi yake na Marekani muda wa kuwa vikwazo vya uchumi vinaendelea.

“Awali tuliingia katika mazungumzo tukikabiliwa na vikwazo. Hatutafanya hivyo tena. Simamisheni vikwazo na rejeeni katika makubaliano tuliofikia ili mazungumzo yafunguliwe tena,” amesema hayo katika mkutano wa Umoja wa Mataifa.

Marekani iliweka vikwazo ikilenga sekta kuu ya mafuta ya Iran baada ya kujitoa kwenye mkataba wa 2015 ambao ulikuwa unaidhibiti programu ya nyuklia ya Iran.

Uongozi wa Trump ulisema kuwa makubaliano kati ya Iran na mataifa yenye nguvu zaidi haukujitosheleza vya kutosha kuizuia Tehran kutengeneza silaha za nyuklia au kujihusisha na vitendo vinavyoonekana kuhatarisha usalama.

Tehran tangu wakati huo imepitiliza viwango vilivyokuwa vimewekwa katika mkataba wa 2015 katika uzalishaji wa nyuklia, wakidai kuwa pande zilizosaini mkataba huo hauheshimu makubaliano hayo waliofikia na Iran, hususan suala la kuhakikisha kuwa vikwazo dhidi yake vinapunguzwa.

XS
SM
MD
LG