Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 12:45

Putin afuatilia mazoezi ya kimkakati ya nyuklia akijitayarisha kujibu 'shambulizi kubwa la nyuklia'


Russia ikifanya mazoezi ya silaha za kimkakati za nyuklia hali inayohatarisha kutokea vita vya nyuklia katika vita yake na Ukraine.
Russia ikifanya mazoezi ya silaha za kimkakati za nyuklia hali inayohatarisha kutokea vita vya nyuklia katika vita yake na Ukraine.

Utawala wa Kremlin ulisema Rais wa Russia Vladimir Putin Jumatano akiwa masafa ya mbali alifuatilia mazoezi ya majeshi ya kimkakati ya silaha za taifa za nyuklia  ambayo yalikusudia kufanya majaribio ya kujibu “shambulizi kubwa la nyuklia” dhidi ya nchi yake.

Televisheni ya Russia ilionyesha video ya Putin akiangalia mazoezi hayo katika televisheni kubwa, huku kukiwa na maoni kutoka kwa viongozi wa kijeshi. Katika matangazo hayo, Waziri wa Ulinzi wa Russia Sergei Shoigu alisema mazoezi hayo yalihusisha a nyambizi zenye kubeba silaha za nyuklia, ndege ya masafa marefu na mazoezi ya urushaji wa makombora ya balistiki na makombora ya masafa marefu.

Rais wa Russia Vladimir Putin Jumatano akiwa masafa ya mbali akifuatilia mazoezi ya majeshi ya kimkakati ya silaha za taifa za nyuklia, Moscow, Oct. 26, 2022. (Pool photo)
Rais wa Russia Vladimir Putin Jumatano akiwa masafa ya mbali akifuatilia mazoezi ya majeshi ya kimkakati ya silaha za taifa za nyuklia, Moscow, Oct. 26, 2022. (Pool photo)

White House ilisema Jumanne kuwa Russia ilikuwa imetoa taarifa kuwa itafanya mazoezi ya kila mwaka, yanayoitwa “Grom” au “Thunder.” Mazoezi hayo yamekuja wakati NATO imeanza mazoezi ya kila mwaka ya silaha za nyuklia, yajulikanayo kama “Steadfast Noon,” siku ya Jumatatu.

Kwa siku kadhaa, maafisa wa Russia walikuwa wanadai kuwa Ukraine inapanga kutengeneza na kutumia kile kiitwacho “bomu chafu” katika vita vyake na Russia.

Mabomu machafu yanatengenezwa kwa vilipuzi vya kawaida na malighafi zenye miale ya nyuklia ambayo yanaweza kusababisha vifo vya watu wengi na kuharibu mazingira.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limejadili shutuma za Russia katika mkutano wa faragha Jumanne.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipokutana New York kujadili mgogoro wa Russia-Ukraine, Octoba 21, 2022.
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipokutana New York kujadili mgogoro wa Russia-Ukraine, Octoba 21, 2022.

Ukraine na washirika wake wa Magharibi wamekanusha madai hayo kwa nguvu zote na wanadhani wanatumika kama chambo cha aina fulani cha kukuza vita huko Ukraine.

Akizungumza kutoka makao makuu ya ushirika huo mjini Brussels Jumatano, Katibu Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg ameziita tuhuma hizo “upuuzi” na “uongo wa dhahiri,” na kuionya Russia kutotumia kisingizio cha uongo kukuza vita hivyo.

Rais wa Marekani Joe Biden ametoa onyo kama hilo Jumanne. Alipoulizwa na waandishi iwapo alifikiria Russia ilikuwa inatumia kisingizio cha bomu chafu kuweka ishara ya uongo ya operesheni na kutumia bomu lake chafu, alisema, “Russia itakuwa inafanya kosa la kustaajabisha ikiwa itatumia mbinu ya silaha za nyuklia.”

Mwandishi wa UN amechangia katika habari hii.

XS
SM
MD
LG