Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 23:35

Marekani kuanzisha uchunguzi dhidi ya kampuni ya Google


Idara ya Sheria ya Marekani inajiandaa kuichunguza kampuni ya Aphabet Inc Google ikitafuta kujua iwapo kigogo huyo wa teknolojia amevunja mkusanyiko wa sheria mbalimbali za ushindani zilizowekwa na serikali kuu na jimbo.

Vyanzo viwili vya habari vinavyojua kadhia hiyo vimethibitisha kuwepo uchunguzi huo na vimeeleza kuwa sheria hiyo inaitaka kampuni hiyo kuheshimu sheria hiyo ya ushindani inayotoa fursa sawa kwa wote katika kuendesha shughuli zake pana za biashara ya mitandaoni,

Maafisa wa Idara ya Sheria, kitengo kinachosimamia sheria hiyo na Tume ya Biashara ya Serikali Kuu (FTC), ambazo zote zinasimamia sheria ya ushindani unaotoa fursa sawa katika kufanya biashara, walikutana wiki za hivi karibuni kuibana kisheria Google, vyanzo hivyo vimesema wakitaka wasitajwe majina yao kwa sababu hawana ruhusa kutoa taarifa hizo rasmi.

Uwezekano wa kuwepo uchunguzi huo ni dalili ya ukosoaji dhidi ya kampuni hiyo uliofanywa na uongozi wa Rais wa Marekani Donald Trump, ambaye amezituhumu kampuni za mitandao ya kijamii na Google kwa kuzikandamiza sauti zenye sera za kikonsavativu katika safu zao zilizoko mitandaoni.

Chanzo kimoja kimesema uwezekano wa kufanyika uchunguzi huo, kwanza uliripotiwa na Jarida la Wall Street, likiangaza tuhuma zilizoelekezwa kwa Google kuwa inatoa kipaumbele kwa biashara zake katika ingini za mitandaoni za kutafuta habari.

Msemaji wa Idara ya Sheria amesema hawezi kuthibitisha au kukanusha kuwa uchunguzi huo uko katika kutathminiwa iwapo ufanyike au la.

Google ilipotakiwa kutoa maoni yake juu ya kadhia hii ilikataa kusema chochote.

Uchunguzi unaofanywa na FTC

Mapema mwaka 2013, FTC ilifunga uchunguzi wa muda mrefu dhidi ya Google, na kuipa onyo dogo.

Chini ya shinikizo la FTC, Google ilikubali kuacha mwenendo wake wa “kufuta” tathmini na takwimu zinazowekwa na washindani wake katika tovuti zao kwa ajili ya bidhaa zao wenyewe, na kuruhusu wanaoweka matangazo kuhamisha takwimu kupeleka katika tathmini zinazofanywa na kampeni za kibiashara zinazojitengemea.

Mitandao ya Google Search, You Tube, reviews, maps na biashara nyingine, ambazo kwa upana zaidi zinatumiwa bila malipo yeyote na walaji lakini zinadhaminiwa kupitia matangazo, zimeipaisha juu kutoka kuwa kampuni ya kawaida na kuifanya kuwa kampuni tajiri zaidi kuliko nyingine zilizo tajiri duniani kwa kipindi tu cha miongo miwili.

Lakini katika safari yake hiyo, Google imetengeneza maadui katika ulimwengu wa teknolojia, ambao wamepeleka malalamiko kwa wasimamizi wa sheria juu ya kuhodhi kwake soko, na mjini Washington, ambako wabunge wamelalamika juu ya masuala yanayotokana na madai ya upendeleo wa kisiasa hadi mipango yake kwa ajili ya China.

XS
SM
MD
LG