Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Mei 09, 2024 Local time: 02:50

Mjue Felix Tshisekedi rais ajaye DRC


Felix Tshisekedi, akiwapungia mkono wafuasi wake wa UDPS, Januari 10, 2019
Felix Tshisekedi, akiwapungia mkono wafuasi wake wa UDPS, Januari 10, 2019

Sehemu kubwa ya maisha yake, Felix Tshisekedi yalikuwa yanafunikwa na kivuli cha baba yake Etienne, kiongozi mkongwe machachari wa upinzani aliyekuwa akiingizwa gerezani na kutolewa na kutumikia serikali, katika kipindi takriban cha miaka 60 ya harakati zake za siasa mpaka alipofariki mwaka 2017.

Baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa uchaguzi wa urais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo saa chache Alhamisi asubuhi, Tshisekedi mdogo anaonekana yuko tayari kufikia lengo la maisha yake ambalo lilimponyoka baba yake.

“Mimi ni rais wa wananchi wote wa Congo,” Tshisekedi aliwaambia maelfu ya wafuasi wake walio kuwa na furaha, wengi wao walikuwa wameparamia ukuta wa jengo la makao makuu ya chama chake na miti iliyoko nje ya jengo hilo ili waweze kumuona kiongozi huyo aliyekuwa jukwaani.

Kanisa Katoliki linalo heshimiwa nchini Congo, ambalo lilisambaza waangalizi wa uchaguzi 40,000 katika uchaguzi uliofanyika Disemba 30, na kuhitimisha kuwa mgombea aliyekuwa namba mbili, Martin Fayulu, ndiye hasa mshindi wa wazi, kwa mujibu wa wanadiplomasia waliopewa taarifa juu ya yaliyo bainishwa na wachungaji hao katika uangalizi wao.

Felix Tshisekedi
Felix Tshisekedi

Lakini kambi ya Tshisekedi imekanusha kuwa ilifanya makubaliano na Kabila, na kusema mazungumzo yaliyofanyika wakati huo wa uchaguzi na wawakilishi wa Kabila yalikuwa yanakusudia tu kuhakikisha kuna kukabidhiana madaraka kwa amani.

Uchaguzi huo utawezesha kwa mara ya kwanza kwa Congo kukabidhiana madaraka kupitia upigaji kura tangu nchi hiyo ipate uhuru wake kutoka Ubelgiji 1960, baada ya miongo kadhaa ya mapinduzi, udikteta, mauaji na vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Lakini bado kuna shaka juu ya ushindi wa Tshisekedi na wasiwasi iwapo ataweza kuzuia machafuko mapya – kwani watu wasio pungua wanne wameripotiwa kuuwawa katika maandamano yaliyo fanywa na wafuasi wa Fayulu huko upande wa magharibi Alhamisi – na iwapo atakuwa na amri ya kutekeleza ahadi zake za kampeni za kupambana na ufisadi.

Mpasuko ndani ya Chama

Tangazo la tume ya uchaguzi lilimnyanyua mara moja mtu ambaye mpaka siku za hivi karibuni, alikuwa hana mvuto mkubwa katika siasa za Congo.

Ni moja kati ya watoto watano, Tshisekedi, 55, alikua katika mji mkuu Kinshasa katika miaka ya awali ya utawala wa Mobutu Sese Seko ambaye aliipa nchi hiyo jina la Zaire.

Baba yake Tshisekedi alitumikia katika serikali ya Mobutu kabla ya kutofautiana na kuanzisha chama chake cha UDPS, ambacho ndio upinzani wa kwanza kuundwa Zaire, mwaka 1982.

UDPS ilivumilia ukandamizaji wa kinyama, na baba yake Tshisekedi alifungwa jela mara nyingi. Felix aliondoka na mama yake na ndugu zake kwenda Ubelgiji 1985, ambapo alifanya kazi za kawaida.

Kuibuka kwa Felix

Félix Tshisekedi
Félix Tshisekedi

Alikuwa mwanachama wa UDPS lakini alikuwa anajituma katika hali ya kujificha mpaka 2011, aliposhinda nafasi ya ubunge wa taifa katika uchaguzi uliofanya baba yake kuwa wapili katika uchaguzi ambao kabila alishinda. Lakini chama kilisema kuwa matokeo ya uchaguzi yalikuwa yamechakachuliwa.

Akiwa katika utu uzima afya ya Tshisekedi ilitetereka katika miaka kadhaa iliofuatia na alitumia muda wake mwingi huko Ulaya akifanya matibabu, Felix alijiongeza katika wasifu wake, na kutembelea maeneo kadhaa ya ndani ya Congo 2014.

Alikabiliwa na upinzani ndani ya chama, wanachama ambao walikuwa wanamkosoa Kabila kwa kurithi urais kutoka kwa baba yake, Laurent Kabila, aliye uwawa 2001. Baadhi yao walimtuhumu Felix na mama yake kwa kukifanya chama hicho kama ni himaya ya familia yao.

Baadhi ya viongozi wa chama walikuwa hususan na wasiwasi mwaka 2015 wakati Felix alipokubali kufanya mazungumzo na wawakilishi wa Kabila ambao walikuwa na lengo la kuzungumzia kipindi cha mpito kitakacho mwezesha Kabila kubakia madarakani wakati muda wake wa kuwepo madarakani utakapo malizika 2016.

Kifo cha Etienne

Etienne Tshisekedi
Etienne Tshisekedi

Kifo cha Etienne Februari 2017, mara baada ya chama kukubali Kabila aendelee kushikilia madaraka kwa mwaka moja zaidi baada ya maandamano yakutisha, ambayo yalimsukuma Felix katika nafasi ya juu katika upinzani.

Tabia yake ya upole na kufanana kwake na Etienne – tangu maumbile mpaka kofia yake maarufu ambayo hakuacha kuivaa- ilimsaidia kukonga nyoyo za wengi, viongozi na wanachama wa kawaida katika chama hicho.

Lakini, bado baadhi ya viongozi wa muda mrefu wa chama hicho walikuwa wakinung’unika kisiri kwamba Etienne hana uwezo wa baba yake Etienne, ambaye mwili wake uko katika nyumba ya kuhifadhia maiti Brussels kwa miaka miwili kwa sababu serikali ilichelea kuwa kurudishwa kwake nchini Congo kutaleta maandamano.

Muungano na Fayulu

Mnamo Novemba, alikubali kumuunga mkono Fayulu katika uchaguzi wa urais ili kuupa upinzani fursa bora zaidi ya kumshinda mgombea ambaye alichaguliwa na Kabila amrithi. Lakini saa 24 baadae, alijitoa kutoka katika mkataba huo, akidai kuwa wafuasi wake walimtaka agombee yeye mwenyewe.

Iwapo ushindi wake utapitishwa na ataapishwa kuchukua madaraka baadaye mwezi huu, atakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo mahitaji ya wananchi wa Congo milioni 13 wanaohitaji chakula cha msaada, manung’uniko juu ya uhalali wa ushindi wake ambao unaweza kuhamasisha wapiganaji upande wa mashariki.

XS
SM
MD
LG