Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 11, 2024 Local time: 05:21

Misri yawakamata madaktari wanaokosoa hali ya maambukizi ya COVID-19


Rais Abdel Fattah el-Sissi
Rais Abdel Fattah el-Sissi

Daktari mmoja amekamatwa baada ya kuandika makala juu ya mfumo mbovu wa wafya nchini Misri.

Na mfamasia mmoja alikamatwa kutoka ofisini kwake baada ya kuposti kuwepo kwa upungufu wa vifaa vya kujikinga.

Naye Mhariri alichukuliwa kutoka nyumbani kwake baada ya kudadisi takwimu rasmi za maambukizi ya virusi vya corona. Daktari mjamzito amekamatwa baada ya rafiki yake kutumia simu yake kuripoti maambukizi ya virusi vya corona yaliyokuwa hayajathibitishwa.

Wakati mamlaka nchini Misri inajitahidi kuzuia kuenea kwa mlipuko wa virusi vya corona, vyombo vya usalama vimejaribu kukandamiza ukosoaji jinsi serikali ya Rais Abdel Fattah el-Sissi inavyoshughulikia mgogoro wa afya.

Siyo chini ya madaktari 10 na waandishi wa habari sita wamekamatwa tangu mlipuko wa virusi vya corona kuikumba Misri mwezi Februari, kwa mujibu wa makundi ya haki za binadamu. Wafanyakazi wengine wa afya wanasema wameonywa na viongozi wao kukaa kimya au kuadhibiwa.

Mwandishi wa habari wa kigeni amelazimika kukimbia, akihofia kukamatwa, na wengine wawili wameitwa na kukaripiwa kwa “kukiuka weledi wa uandishi.”

Maambukizi ya virusi vya corona yanaendelea kuongezeka nchini Misri yenye takriban watu milioni moja, na kutishia kuwa hospitali huenda zikaelemewa. Hadi Jumatatu, Wizara ya Afya ilikuwa imerikodi maambukizi 76,253, vifo 3,343 – idadi ya juu kabisa ya vifo katika ulimwengu wa kiarabu.

“Kila siku ninakwenda kazini, ninajitolea maisha yangu na maisha ya familia yangu,” amesema daktari aliyeko mstari wa mbele katika kutibu virusi vya corona mjini Cairo, ambaye alizungumza kwa sharti jina lake lihifadhiwe kwa kuogopa kulipiziwa kisasi, kama ilivyokuwa kwa madaktari wengine wote waliotoa maelezo katika habari hii. “Baadae waliwakamata marafiki zangu kutuletea ujumbe. Sioni mwanga mbele yetu.”

Mwaka 2013, el-Sissi, akiwa waziri wa ulinzi, aliongoza jeshi kumuondoa rais wa kwanza aliyechaguliwa kidemokrasia, Mohamed Morsi, baada ya utawala wake wa muda mfupi ulizusha maandamano ya nchi nzima. Katika miaka iliyofuatia, el-Sissi amekuwa akiwakamata waasi, akiwafunga wapinzani wa siasa za Kiislam, wanaharakati wa kiraia, waandishi wa habari na wanawake wacheza dansi.

Hivi sasa kamata kamata imeelekezwa kwa madaktari ambao wanazungumza wazi juu ya uhaba wa vifaa vya kujikinga au kudadisi idadi rasmi ya maambukizi ya virusi vya corona.

XS
SM
MD
LG