Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 12:14

Miongo miwili baada Diallo kuuawa New York, mama yake bado anamatumaini 


Kadiatou Diallo, kushoto, akitembelea kaburi la Emmett Till huko Alsip, Ill., Agosti. 28, 2015, kumuenzi. Mauaji ya kijana huyu miaka 60 iliyopita huko Mississippi yaliimarisha harakati za haki za raia Marekani. AP PHOTO
Kadiatou Diallo, kushoto, akitembelea kaburi la Emmett Till huko Alsip, Ill., Agosti. 28, 2015, kumuenzi. Mauaji ya kijana huyu miaka 60 iliyopita huko Mississippi yaliimarisha harakati za haki za raia Marekani. AP PHOTO

Ilikuwa ni kilio cha wazi cha George Floyd, picha ya video iliyochukuliwa akionekana amekandamizwa shingo yake na goti la afisa wa polisi ardhini, hiyo lilimuuma Kadiatou Diallo akikumbuka kifo cha mtoto wake ambaye alikuwa bado kijana mdogo. 

“Alikuwa anamlilia mama yake,” alisema mwanamke huyo. “Nilimsikia kama mama wa Amadou Diallo. Na kina mama wote walisikia kilio chake.”

Miaka 21 kabla ya kifo cha Floyd Mei 25 huko Minneapolis, Minnesota, maafisa wa polisi wanne wa Jiji la New York walimpiga risasi kadhaa kijana mdogo zaidi Diallo katika eneo lisilokuwa na mwanga la nyumba alimokuwa anaishi katika mji wa Bronx.

Maafisa hao baadae walidai kuwa walimfananisha kwa makosa na mhamiaji mwenye umri wa miaka 23 kutoka Afrika Magharibi kwa kushukiwa kubaka na hivyo walimpiga risasi kujihami wakati alipotoa kitu cheusi ambacho walifikiria ni bastola. Ilikuwa ni pochi ya kuhifadhi fedha.

Kifo cha kijana huyu mdogo mweusi Februari 4, 1999, na kuachiwa kwa maafisa wazungu baada ya kufunguliwa mashtaka ya mauaji ya daraja la pili mwaka mmoja baadae, kulisababisha wimbi la maandamano kupinga uamuzi huo. Ilimleta mama yake mwenye majonzi kutoka Guinea na kumfanya hatimaye mwanamke huyo mfanyabiashara kubadilika kuwa mwanaharakati akitaka mageuzi katika jeshi la polisi, usawa wa kijamii na elimu.

“Mtoto wangu, mwanangu wa kwanza, Amadou Diallo, alipigwa risasi bila ya sababu,” mama wa watoto watatu wakubwa sasa wanaoendelea kuishi aliiambia VOA kwa njia ya mahojiano kupitia mtandao wa Skype mapema Juni.

Kadiatou Diallo, na mwanawe Amadou Diallo
Kadiatou Diallo, na mwanawe Amadou Diallo


Kadiatou Diallo ameeleza kuwa kifo cha mwanawe, kama kile cha Floyd, ni “ni kielelezo cha wakati tulioko katika historia.” Amesema kiliwasukuma watu “wa rangi na itikadi zote kuandamana kwa mshikamano na kudai maelezo, ‘Vipi binadamu anaweza kupigwa risasi mara 41?’” Kati ya hizo risasi 19 zilimpata Diallo.

Kesi yake ilikuwa imepewa umaarufu mkubwa, ambapo mashtaka dhidi ya maafisa wa polisi yalirushwa kupitia TV ya mahakama. “Ulimwengu mzima uliangalia kesi hiyo,” Kadiatou Diallo alisema.

Diallo aliingizwa katika kumbukumbu ya wimbo wa Bruce Springsteen,” American Skin (41 Shots).” Mtandao wa Netflix “Ulionyesha Makala kadhaa juu ya kesi hiyo zilizojulikana kama “Trial by Media” zikipitia tena habari ya mauaji hayo katika toleo maarufu mwezi May.

‘Niliomba watu wawe watulivu’

Wakati hukumu ilipotangazwa Februari 2000, Kadiatou Diallo aliegemea katika imani yake ya Kiislam kuzungumza na waandishi wa habari.

“Niliomba kuwepo na utulivu na maombi,” anakumbuka hilo. “Niliwaambia wote, ‘Uvunjifu wa amani usisababishe uvunjifu zaidi wa amani. Amadou alikabiliwa na uvunjifu mkubwa wa amani.’ Lakini niliendelea kuwa na ari yangu, na nimewaambia watu kuwa nitaendelea kupigania usawa, haki na haki ya kuishi.

Hapo kabla, kama ilivyo hivi sasa, Kadiatou Diallo anajaribu kutafuta mambo mazuri katikati ya balaa hii, akigeuza maumivu na hasira kuwa ni vitendo vinavyojenga.

Baada ya mama huyo na mtalaka mume wake kupokea fidia ya dola milioni 3 kutoka Jiji la New York kwa mtoto wao kuuawa kwa makosa, aliandika na mwenza wake kumbukumbu inayoitwa “My Heart Will Cross This Ocean.”

Alianzisha Taasisi ya Amadou Diallo, isiyoingiza faida huko New York ambayo inahamasisha maridhiano ya tofauti za rangi na fursa za elimu ya juu. Inatoa msaada wa malipo katika vyuo mbalimbali mjini New York kwa wahamiaji au wanafunzi wenye asili ya Kiafrika. Inaendesha kituo cha elimu katika mji wa pili kwa ukubwa, Labe huko Guinea. Taasisi hiyo pia inalenga “kuunganisha mgawanyiko uliopo kati ya vijana wa kiafrika wanaoishi ughaibuni na wale wanaoishi Afrika,” amesema mwanamama huyo.

Tovuti ya Kigoda hicho inaonyesha picha kamili ya Diallo. Kadiatou Diallo alisema ilimuumiza sana kusikia mwanawe akielezwa – katika mahakama na habari mbalimbali zilizochapishwa – kama ni mfanyabiashara mhamiaji wa mtaani.

Alikuwa ni kijana aliyeelimika, anazungumza lugha mbalimbali na amesafiri ulimwenguni, alikulia Liberia, Guinea, Togo na Thailand. Alihamia Marekani Septemba 1996. Katika mazungumzo yao ya mwisho ya simu, Kadiatou Diallo alisema, aliwajulisha kuwa ameweza kuweka akiba ya dola 9,000 na amejiandikisha kujiunga na chuo kimojawapo kuanza masomo. “Nitakufanya ujivunie mafanikio yangu,” alimwambia mama yake.

Siku nne baadae aliuawa.

Mama yake Diallo na mwanawe
Mama yake Diallo na mwanawe

Kifo cha Diallo chaacha Athari

Mauaji ya Diallo yaliangaza Kitengo cha Polisi cha New York, Idara Inayohusika na Jinai za Mitaani, ambako maafisa hao wanne walikuwa wanatumikia. Idara hiyo ilivunjwa mwaka 2002 katikati ya uchunguzi uliokuwa ukifanywa na serikali kuu juu ya madai ya uvunjaji wa haki za binadamu na ubaguzi kwa kuwasimamisha bila sababu njiani na kuwahoji watu wa rangi na waafrika.

Wakati huohuo, Kadiatou Diallo anaendelea kushinikiza kuwepo mabadiliko – kwa upande mmoja kupitia Kamati za Sheria, taasisi ya ngazi za chini New York zinazopinga vitendo vya uvunjifu wa amani vya polisi na kusudio (lengo) lao ni kuwapa nguvu watu wa rangi mbalimbali.

Ni sehemu ya muungano juhudi zao zilipelekea Gavana wa New York Andrew Cuomo kuidhinisha mwezi huu mapendekezo ya mageuzi katika jeshi la polisi ikiwemo kupiga marufuku kukandamiza shingo ya mtuhumiwa ardhini kwa goti na kuruhusu uwazi wa rekodi za nidhamu za maafisa wa polisi.

Barua ya wazi ya Kamati ya Sheria ya Juni 14 kwa Cuomo ilimkemea kuchukuwa sifa kwa mageuzi “ambazo sisi familia tulisaidia kuhamasisha katika miaka kumi iliyopita,” na kumtuhumu anazuia maendeleo. Jina la Diallo ni la kwanza kati ya 18 walioordheshwa kusaini mageuzi hayo.

Taasisi ya Amadou Diallo iliwasiliana na jeshi la polisi. Mmoja wa mwanachama wake wa bodi ni Graham Weatherspoon, ambaye ni mstaafu kutoka Kitengo cha Polisi cha New York.

Matarajio ya mabadiliko

Hatua za kukabiliana na kifo cha Floyd cha hivi karibuni na vifo vya Wamarekani Weusi wengine, Kadiatou Diallo anaona kuna muamko mpana mpya wa kuzungumzia tatizo la usawa wa rangi.

“Naamini mtoto wangu alifungua mlango wakati ule, miaka 21 iliyopita,” ukatili wa polisi na ubaguzi wa rangi kuchunguzwa, amesema mama huyo.

“Tofauti iliyoko leo ni mitandao ya kijamii” na picha za video zinazoweza kupigwa na kila mtu, “ ili ulimwengu uone namna George Floyd alivyouawa. Kama ingelikuwa hakuna picha ya video ingekuwaje? Habari hiyo ingelikuwa ya namna gani?”

Aliendelea kusema, “Hali hii ya sauti nyingi kupazwa, hawa vijana wanaoshikana mikono na kuandamana, wakilaani na kudai haki, wanasema Uhai wa Mtu Mweusi unathamani, kila uhai unathamani – Hili ni jambo hata makampuni makubwa hawalipuuzi hivi leo.

“ Ni lazima tutafute ufumbuzi – ufumbuzi wa kudumu- kutatua tatizo hili” la kukosekana usawa, amesema. La sivyo, sijui tunaelekea wapi kuanzia hapa.”

XS
SM
MD
LG