Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 22:56

Waandamanaji duniani waunga mkono maandamano ya Marekani


Waandamanaji New Zealand wakiomboleza kifo cha George Floyd mkazi wa Minneapolis na kulaani kifo chake nje ya Bunge huko Wellington Juni 1, 2020. (Photo by David Lintott / AFP)
Waandamanaji New Zealand wakiomboleza kifo cha George Floyd mkazi wa Minneapolis na kulaani kifo chake nje ya Bunge huko Wellington Juni 1, 2020. (Photo by David Lintott / AFP)

Maelfu ya watu huko New Zealand waliandamana Jumatatu kuunga mkono maandamano yanayoendelea Marekani kulaani kifo cha Mmarekani mweusi George Floyd akiwa chini ya ulinzi wa polisi.

New Zealand

Waandamanaji mjini Auckland walielekea hadi Ubalozi mdogo wa Marekani huku wakiimba kauli mbalimbali zinazotumiwa na waandamanaji Marekani, ikiwemo “maisha ya mtu mweusi muhimu” na “hakuna haki hakuna amani.”

Brazil na Canada

Maandamano ya Jumatatu yanafuatia yale yaliofanyika Jumapili nchini Uingereza, Brazil, Canada na nchi nyingine.

London

Maelfu ya waandamanaji walikusanyika katikati ya mji wa London kupaza sauti kuonyesha uungaji mkono wao kwa wenzao wa Marekani ambao wamejitokeza kulaani vitendo vya polisi tangu kutokea kifo cha Floyd wiki iliyopita huko mjini Minneapolis, jimbo la Minnesota.

Kifo cha George Floyd

Floyd alifariki baada ya afisa wa polisi mzungu Derek Chauvin kuweka goti lake nyuma ya shingo ya mshukiwa kwa zaidi ya dakika nane, hata pale Floyd aliporejea mara kadhaa kumwambia afisa huyo hawezi kupumua.

Waandamanaji nchini Denmark walitembea hadi Ubalozi wa Marekani mjini Copenhagen Jumapili, wakibeba mabango yakiwa na ujumbe mbalimbali kama vile “Acheni Kuwaua Watu Weusi.” Nchini Ujerumani, waandamanaji walibeba ujumbe unaosema, “Wawajibisheni Askari,” na “Nani Unamwita Wakati Polisi Anapouwa?”

Serikali za Kiimla

Katika nchi zenye serikali za kiimla, maafisa wamekosoa vitendo vya polisi hao wakati vyombo vya habari vinavyodhibitiwa na serikali vimeonyesha maandamano kwa kiwano cha malalamiko ya serikali ya Marekani juu ya kukamatwa kwa waandamanaji katika nchi nyingine, kama vile China inavyowatendea waandamanaji wanaounga mkono demokrasia huko Hong Kong.

China

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje wa China Zhao Lijian amesema Jumatatu wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuwa kukosekana utulivu Marekani kunaonyesha “ukubwa wa tatizo la ubaguzi na uhalifu wa polisi nchini Marekani.”

Hilo lilifuatia maoni ya Hu Xijin, Mhariri wa gazeti la Global Times la chama tawala cha kikomunisti cha China, CCP, aliyesema maafisa wa Marekani sasa wanaweza kuona maandamano nje ya madirisha yao : “Nataka kumuuliza Spika wa Baraza la Wawakilishi [Nancy] Pelosi na Waziri [wa Mambo ya Nje Mike] Pompeo: Je, Beijing iwaunge mkono waandamanaji wa Marekani, kama mnavyowatukuza wafanya ghasia Hong Kong?”

Iran

Nchini Iran, ambapo serikali katika miaka ya karibuni imetumia hatua kandamizi kuwakamata waandamanaji nchini humo, televisheni ya serikali imerejea kuonyesha picha za ghasia nchini Marekani. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje Abbas Mousavi ametaka jeshi la polisi nchini Marekani “kuacha kuwatendea uovu watu wenu na kuwaruhusu wapumue.”

XS
SM
MD
LG