Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 05:31

Umoja wa Afrika walaani 'mauaji' ya Mmarekani mweusi Floyd


Mkuu wa Tume ya Umoja wa Afrika, Moussa Faki Mahamat,
Mkuu wa Tume ya Umoja wa Afrika, Moussa Faki Mahamat,

Wakati mji wa Minneapolis ukiteketea kwa moto kutokana na polisi kumuua George Floyd na mshtuko na hali ya kushangazwa ikikua Afrika, baadhi ya balozi za Marekani katika bara la Afrika zimechukua hatua zisizo za kawaida kutoa matamko ya kukosoa tukio hilo, wakisema hakuna mtu aliyekuwa juu ya sheria.

Taaria hizo zilitolewa wakati mkuu wa Tume ya Umoja wa Afrika, Moussa Faki Mahamat, amelaani “mauaji” hayo ya Floyd na kusema Ijumaa taasisi hiyo ya Afrika inapinga “vitendo vya ubaguzi vinavyoendelea dhidi ya raia weusi wa Marekani.”

Afrika haijawahi kushuhudia maandamano ya aina hii ambayo yamezuka kote Marekani, lakini Waafrika wengi wameelezea kuchukizwa na kusikitishwa waziwazi wakijiuliza ni lini Marekani itaweza kufuata njia sahihi.

“Mchora vibonzo vya kisiasa wa Kenya Patrick Gathara alituma ujumbe wa tweet “Ujinga gani unaendelea? ‘Wizi wa ngawira unapoanza ndipo na upigaji risasi nao unaanza? Kenya pia inatatizwa na vitendo vya ukatili vya polisi. Gathara, kama wengine, walikerwa na ujumbe huo wa tweet uliotumwa na Rais Donald Trump, ambao ulikosolewa na kampuni ya Twitter kuwa unavunja sheria kwa “kutukuza uvunjifu wa sheria,” ambapo baadae rais alisema ameeleweka vibaya.

Kwa kuzingatia taswira ya Marekani katika bara hilo ambapo ushawishi wa China unakua na ambapo wengi wanahisi waziwazi uongozi wa Trump hauijali Afrika, baadhi ya wanadiplomasia wa Marekani wamejaribu kudhibiti hali hii.

Balozi wa Marekani nchini Congo, Mike Hammer, akinukuu ujumbe wa tweet kutoka kwa mjasiriamali wa vyombo vya habari nchini humo aliyemtumia ujumbe huo akisema, “Balozi, nchi yako inatia aibu.

Amerika ilio na fahari, ambayo ilipitia hatua mbalimbali kuanzia ubaguzi hadi kumchagua Barack Obama, hadi hivi leo haijaweza kutokomeza uovu wa kishetani wa ubaguzi. Ni watu weusi wangapi wanatakiwa wauawe na maafisa polisi wazungu kabla ya vyombo vya serikali kuchukua hatua thabiti?”

Jibu la Balozi huyo, kwa Kifaransa : “Ninatatizwa sana na kifo kibaya cha George Floyd huko Minneapolis. Wizara ya Sheria inafanya uchunguzi kamili wa jinai ikiwa ni kipaumbele chao. Vikosi vya usalama duniani ni lazima viwajibishwe. Hakuna yeyote aliyekuwa juu ya sheria.”

Taarifa kama hizo pia zilitumwa katika ujumbe wa tweet na balozi za Marekani nchini Kenya na Uganda, wakati balozi za Tanzania na Kenya zilituma ujumbe wa pamoja kutoka ofisi ya Wizara ya Sheria ya Minnesota juu ya uchunguzi unaofanyika.

Viongozi wa Afrika pia walipaza sauti hadharani mwezi uliopita juu ya ubaguzi nchini China, wakati Waafrika walipolalamika kutolewa majumbani na kudhalilishwa katika mji wa Guangzhou wakati janga la COVID-19 likiendelea.

Wakati huo, Marekani mara moja ilijitokeza na kukosoa, ubalozi wake mjini Beijing ukituma tahadhari muhimu ya kiusalama iliyosema “Ubaguzi dhidi ya Wamarekani-Weusi mjini Guangzhou” na kugusia vitendo vinavyo fanywa dhidi ya watu wanaofikiriwa kuwa Waafrika au na mahusiano na Afrika.

Hivi sasa gazeti la China Daily la serikali toleo la Afrika linatuma ujumbe wa tweet ukiwa na picha za video kutoka Minneapolis zenye hashtags #GeorgeFloydWasMurdered and #BlackLivesMatter (GeorgeFloydAliuawa) na (MaishaYaWatuWeusiNiMuhimu).

XS
SM
MD
LG