Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 12:02

Burundi: Rwasa awasilisha kesi mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi


Kiongozi wa chama cha upinzani nchini Burundi Agathon Rwasa.
Kiongozi wa chama cha upinzani nchini Burundi Agathon Rwasa.

Kiongozi wa upinzani nchini Burundi, Agathon Rwasa, Alhamisi aliwasilisha kesi mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais uliofanyika wiki jana. 

Katika hoja yake aliyowasilisha kwenye mahakama ya Katiba mjini katika mji mkuu, Bujumbura, Rwasa anasema ana ushahidi wa kutosha kuonyesha kwamba zoezi hilo liligubikwa na dosari za kila aina.

Punde tu baada ya kuwasilisha malalamishi yake mahakamani, Rwasa aliwaambia waandishi wa habari kwamba kulikuwa na udanganyifu wa wazi katika wilaya na mikoa yote nchini.

"Kulikuwa na dosari kote nchini. Mikoa yote na hata wilaya zote. Uchaguzi uligubikwa na udanganyifu," alisema mwanasiasa huyo.

Kwa mujibu wa sheria za taifa hilo la Afrika Mashariki, mahakama ya Katiba ina hadi tarehe 5 mwezi Juni kuamua kesi hiyo.

Tume ya uchaguzi ilitangaza Jumatatu wiki hii kwamba Jenerali mstaafu Evariste Nayishimiye, ambaye aligombea urais kwa tikiti ya chama kinachotawala CNDD FDD, aliibuka mshindi wa uchaguzi huo wa Jumatano, akiwa na asili mia 69 ya kura zote zilizopigwa.

Tume hiyo ilisema Rwasa, kiongozi wa chama cha upinzai CNL, alipata asili mia 24 ya kura.

Chama cha CNDD FDD kinashikilia kwamba uchaguzi huo ulikuwa wa haki na huru, licha ya wadau mbalimbali kutokubaliana na msimamo huo.

XS
SM
MD
LG