Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 14:38

Maelfu ya wafungwa waachiwa huru Zimbabwe


Wafungwa wakitoka gerezani huko Harare, tarehe 17 Aprili 2021 baada ya msamaha wa rais. Picha na Jekesai NJIKIZANA / AFP.
Wafungwa wakitoka gerezani huko Harare, tarehe 17 Aprili 2021 baada ya msamaha wa rais. Picha na Jekesai NJIKIZANA / AFP.

Kiasi cha theluthi moja ya wafungwa wote nchini Zimbabwe waliachiliwa huru siku ya Alhamisi chini ya msamaha wa rais, miezi michache sana kabla ya uchaguzi mkuu.

Jumla ya wafungwa 4,270, wengi wao wanaume, waliachiliwa huru, kulingana na idara ya magereza nchini humo, ambayo ilielezea kuachiliwa kwa wafungwa hao ni kama "ishara ya kiungwana" ya rais.

"Tungependa kutoa wito kwa...jamii kwa ujumla kuwathamini na kuwajali wafungwa walioachiliwa," ilisema taasisi ya Huduma za Wafungwa na Magereza nchini Zimbabwe (ZPCS) katika taarifa yake.

"Wale waliodhulumiwa wanahimizwa kusamehe".

Hatua hiyo inapunguza msongamano wa watu katika jela zaidi ya 50 nchini humo, ambazo zina uwezo wa kuhudumia watu wapatao 17,000 lakini zimekuwa zikiwashikilia zaidi ya mahabusu 22,000 kabla ya msamaha huo kutolewa.

Hata hivyo, msemaji wa ZPCS Meya Khanyezi aliliambia shirika la habari la AFP "sababu si kupunguza msongamano".

"Hii ilikuwa nia nzuri tu ya rais," alisema.

Msamaha huo umetolewa kwa makundi mbalimbali ya wafungwa wakiwemo wale waliotumikia angalau robo tatu ya vifungo vyao, au moja ya kumi ikiwa walihukumiwa vifungo vya zaidi ya miaka 60.

Msamaha huo hauwahusishi wahalifu wanaotumikia vifungo kwa wizi, uhaini na kuvuruga amani kwa umma na makosa ya usalama.

Wale walioachiliwa wataweza kupiga kura katika uchaguzi wa rais na wabunge ambao utafanyika mwezi Agosti, ingawa tarehe ya uchaguzi bado haijatangazwa.

Rais alishatoa msamaha kama huo katika kilele cha janga la Covid-19 mwaka 2020 kwa nia ya kupunguza kuenea kwa virusi katika mahabusu.

Chanzo cha habari hii ni Shirika la habari la AFP

XS
SM
MD
LG