Mwenyekit wa IEBC, Wafula Chebukati amesema ingawaje maandalizi ya uchaguzi yanaendelea vizuri lakini katika mazingira ya sasa ni vigumu kuandaa uchaguzi huru na wa haki kama hapatakuwa na mabadiliko.
Amesema pia kwamba maafisa wa tume waliotajwa kuhusika kuvuruga uchaguzi wa kwanza tarehe 8 Agosti kwa namna yoyote wanafaa kujiuzulu.
Tamko hilo limekuja saa chache baada ya Kamishna Dkt Roselyn Akombe kutangaza kujiuzulu akiwa Marekani na vyanzo vya habari vimesema kuwa amesema hana mpango wowote wa kurejea Kenya hivi karibuni.
IEBC ilimtangaza Rais Kenyatta kuwa mshindi wa uchaguzi Agosti 8, 2017, akiwa amemshinda mpinzani wake Raila Odinga wa muungano wa upinzani Nasa kwa zaidi ya kura 1.4 milioni.
Odinga alipinga matokeo hayo mahakamani na Mahakama ya Juu ilibatilisha matokeo kutokana na kile ilichosema ulikuwa na kasoro, na kutaka uchaguzi huo urejewe tena katika kipindi cha siku sitini.
IEBC ilitangaza uchaguzi ufanyike Oktoba 26 lakini Odinga alijiondoa wiki iliyopita katika kinyang’anyiro hicho akidai kuwa mageuzi hayakutekelezwa IEBC, na hivyo uchaguzi hauwezi kuwa huru na haki.