Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 05:25

Afisa : Watu 3 wauawa, 12 wajeruhiwa katika shambulizi la Tamasha la California


Hali ilivyokuwa wakati wa shambulizi la bunduki katika tamasha la kilimo na chakula California, Marekani, Jumapili 07.28.2019.
Hali ilivyokuwa wakati wa shambulizi la bunduki katika tamasha la kilimo na chakula California, Marekani, Jumapili 07.28.2019.

Maafisa katika jimbo la California wanasema mshambuliaji aliyekuwa na silaha aliwaua watu 3 Jumapili na kuwajeruhi wengine 15 wakati wa tamasha la kilimo na chakula.

Shambulizi hilo lilitokea katika mji wa Gilroy, mkuu wa polisi katika mji huo Scot Smithee anasema mshambuliaji naye aliuawa baadaye na maafisa wa polisi waliokuwa wanalinda usalama kwenye tamasha hilo. Uchunguzi unaendelea ili kujua nini hasa sababu ya shambulizi hilo

Mjumbe wa Baraza la Jiji la Gilroy Dion Bracco ameliambia shirika la habari la The Associated Press idadi hiyo ya waliouawa na kujeruhiwa ni takwimu za awali kufuatia shambulizi la Jumapili.

Walioshuhudia shambulizi hilo wameripoti kuwepo mshituko na kuchanganyikiwa kwa waliokuwepo katika tukio hilo wakati risasi zilipokuwa zinasikika katika tamasha hilo la Gilroy Garlic Festival katika Jiji lenye wakazi 50,000 lilioko takriban maili 80 (kilomita 176) kusini mashariki ya San Francisco.

Shambulizi hilo lilitokea wakati wa tamasha hilo linalofanyika kila mwaka. Ni sherehe za siku tatu zinazoonyesha ushindani wa vyakula na mapishi na muziki zinazowavutia zaidi ya watu 100,000. Jumapili ilikuwa siku ya mwisho ya sherehe hizo.

Rais Donald Trump alituma ujumbe wa tweet kuhusiana na shambulizi hilo la bunduki Jumapili usiku. “Vyombo vya Ulinzi vipo katika tukio la shambulizi huko Gilroy, California. Ripoti zilizopo mshambuliaji bado hajakamatwa. Kuweni waangalifu na salama!” aliandika.

Kituo cha afya cha Stanford kimepokea wagonjwa wawili ambao wanapatiwa matibabu kutokana na shambulizi hilo la Tamasha la Gilroy Garlic Festival, msemaji wa kituo hicho Julie Greicius amesema.

Hata hivyo hakuwa na ufafanuzi zaidi juu ya majeraha au hali zao. Hospitali ya Santa Clara Valley ilipokea majeruhi watano, msemaji Joy Alexiou amesema. Pia alikuwa hana taarifa zozote juu ya hali zao.

XS
SM
MD
LG