Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 09:10

Viongozi wa dunia walaani shambulizi la Sri Lanka lililouwa zaidi ya watu 200


Jeshi la Sri Lankan laweka ulinzi mkali kuzunguka eneo takatifu la Mtakatifu Anthony baada ya mlipuko mjini Colombo, Sri Lanka, Jumapili, April 21, 2019.
Jeshi la Sri Lankan laweka ulinzi mkali kuzunguka eneo takatifu la Mtakatifu Anthony baada ya mlipuko mjini Colombo, Sri Lanka, Jumapili, April 21, 2019.

Watu zaidi ya 200 wameuawa na takriban wengine 450 kujeruhiwa Jumapili ya Sikukuu ya Pasaka kwenye makanisa matatu na hoteli nne nchini Sri Lanka baada ya milipuko mitatu, kati yake kulikuwa na mabomu yakujitoa muhanga.

Wachambuzi wanasema kuwa milipuko hiyo ni mikubwa zaidi kutokea kwenye kisiwa hicho cha Bahari ya Hindi, tangu kumalizika kwa vita vya wenyewe kwa wenyewe miaka 10 iliyopita.

Vyanzo vya habari vimeripoti kuwa washukiwa saba walikamatwa na vyombo vya usalama na wengine watatu kuuawa katika nyumba moja iliyoko mji mkuu wa Sri Lanka, Colombo saa chache baada ya mfululizo wa milipuko hayo, mengine ambayo maafisa wamesema yalikuwa mabomu ya kujitoa muhanga.

Serikali ya Sri Lanka imesema hakuna yeyote au kundi lililojitokeza kudai kuhusika na tukio hilo, na tayari Jeshi limepeleka kikosi kulinda eneo hilo ambapo milipuko hiyo ilitokea.

Viongozi wa Dunia

Rais wa Marekani Donald Trump ametuma salamu za rambirambi kwa watu wa Sri Lanka na iko tayari kutoa misaada kwa nchi hiyo.

Waziri Mkuu wa India Narendra Modi ameeleza masikitiko yake akisisitiza kuwa haikubaliki kabisa kwa unyama huo kufanyika katika nchi hiyo.

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amesema shambulizi hilo ni dhidi ya ubinadamu kwa dunia nzima.

Naye Kiongozi wa Kanisa Katoliki ulimwenguni Papa Francis akiwahutubia maelfu ya watu waliomiminika katika Kanisa la Mtakatifu Petro kusikiliza ujumbe wake wa Pasaka amesema: "Ningependa kuelezea kuguswa wangu kwa jamii hii ya Kikristo iliyolengwa wakati wa maombi yake, na kwa wahanga wote wa mashambulizi ya kikatili ya aina hiyo.

Sri Lanka ilikuwa vitani kwa miongo mingi na wapiganaji waliotaka kujitenga wa Tamil Tigers hadi mwaka wa 2009.

Hali ya Hatari yatangazwa

Serikali imetangaza hali ya hatari na kuwataka watu kutotoka nje mjini Colombo na imefunga mitandao ya kijamii na tovuti ikiwa ni pamoja na Facebook na WhatsApp. Haijafahamika haraka ni lini amri hiyo itaondolewa.

"kwa jumla, tuna habari za vifo vya watu 207 kutoka hospitali zote. Kwa mujibu wa habari hiyo mpaka sasa tuna watu 450 waliojeruhiwa na wamelazwa hospitali,” alisema msemaji wa polisi Ruwan Gunasekera. Karibu watu 27 miongoni mwa waliokufa ni raia wa kigeni.

Waziri Mkuu wa Sri Lanka

Taarifa zinaeleza kuwa hoteli zilizoshambuliwa mjini Colombo ni Shangri-La, Kingsbury, Cinnamon Grand na Tropical Inn karibu na makazi ya wanyama pori. Waziri Mkuu Ranil Wickremesinghe ameitisha mkutano wa baraza la usalama Jumapili.

"Nina laani vikali mashambulizi haya ya uwoga dhidi ya watu wetu. Ninawaomba wananchi wa Sri Lanka wakati huu mgumu kuungana na kuwa imara,” alieleza kupitia ujumbe wake wa Twitter.

Rais wa Sri Lanka

Rais Maithripala Sirisena amesema ameamuru kikosi maalum cha polisi na jeshi kuanza uchunguzi mara moja kutatufa kiina na wahusika wa shambulizi hilo.

XS
SM
MD
LG