Watu zaidi ya 900 wafariki katika tetemeko la ardhi Afghanistan

Watu waliojeruhiwa katika tetemeko kubwa la ardhi wakiondolewa kupelekwa hospitali katika Mkoa wa Paktika, Afghanistan, June 22, 2022, katika picha hii iliyotolewa kutoka katika picha ya video. (Bakhtar News Agency/Handout via Reuters)

Tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 6.1 kwa kipimo cha Rikta limeuwa zaidi ya watu 900 nchini Afghanistan mapema Jumatano, maafisa wa kudhibiti majanga wamesema.

Maafisa hao wameongeza kuwa wengine zaidi 600 walijeruhiwa na idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka wakati maelezo yakiendelea kutolewa kutoka kwenye vijiji vya mbali milimani.

Wameeleza pia kuwa:“ Kwa bahati mbaya kutokana na taarifa za awali watu 920 wamepoteza maisha katika majimbo mbalimbali na wilaya kama vile Paktika , Geian , Nekah, Barmal na Zorwaki , Khost , Esparai, Nangahar, Achene, kutokana na tetemeko la ardhi lililotokea usiku wa jana na watu 610 wamejeruhiwa.”

Picha za vyombo vya habari vya Afghanistan zinaonyesha nyumba zimekuwa vifusi na miili ikiwa imefunikwa na mablanketi chini ardhini .

Helikopta zimepelekwa katika eneo la tukio katika juhudi za uokozi kuwafikia waliojeruhiwa na kupeleka vifaa vya hospitali na chakula, amesema hayo afisa wa wizara ya mambo ya ndani , Salahuddin Ayubi.

Hata hivyo taarifa zinasema kwamba idadi hiyo inaweza kuongezeka katika baadhi ya vijiiji kwenye maeneo ya milima na itachukua muda kupata maelezo zaidi.