Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 15:18

Putin aahidi kuendeleza mashambulizi dhidi ya Ukraine


Rais wa Russia Vladimir Putin
Rais wa Russia Vladimir Putin

Rais wa Russia Vladimir Putin ameahidi Ijumaa kuendeleza mashambulizi dhidi ya Ukraine licha ya Ukraine kujibu mashambulizi hivi karibuni na kuonya kuwa Moscow inaweza kuanza kushambulia miundombinu muhimu ya nchi hiyo iwapo majeshi ya Ukraine yatalenga vituo mbalimbali ndani ya Russia.

Akizungumza na waandishi wa habari Ijumaa baada ya kuhudhuria mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya Ushirikiano wa Shanghai huko Uzbekistan, Putin alisema “ukombozi huo” wa sehemu yote ya mkoa wa mashariki wa Donbas huko Ukraine utaendelea kuwa ni lengo kuu la kijeshi la Russia na haoni haja ya kubadilisha hilo.

“Hatuna haraka,” kiongozi huyo wa Russia alisema, akiongeza kuwa Moscow tayari imepeleka askari wa kujitolea kupigana huko Ukraine. Baadhi ya wanasiasa wenye msimamo mkali na waandishi wa mitandao ya blog ya kijeshi wameihimiza Kremlin kufuata mfano wa Ukraine na waamrishe kuhamasihwa watu kujiunga na mapigano ili kuongeza nguvu za wanajeshi, wakilalamika kuwepo upungufu wa nguvu kazi Russia.

Russia ililazimika kuondoa wanajeshi wake kutoka maeneo makubwa ya kaskazini mashariki ya Ukraine wiki iliyopita baada ya Ukraine kujibu mashambulizi kwa ghafla.

Hatua ya Ukraine kuchukua maeneo kadhaa ya miji na vijiji yaliyokuwa yametekwa na Russia ilikuwa ishara kubwa ya kuemewa kwa majeshi ya Moscow kwani wanajeshi wake walilazimika kurudi nyuma kutoka katika maeneo karibu na mji mkuu mapema katika vita hiyo.

Katika tamko lake la kwanza kufuatia Ukraine kujibu mashambulizi, Putin alisema: “Tuangalie vipi hili litaendelea na vipi litamalizika.”

FILE PHOTO: Kinu cha nishati ya nyuklia cha Zaporizhzhia na moto ulioko katika eneo hilo kutokana na mashambulizi ya majeshi ya Russia.
FILE PHOTO: Kinu cha nishati ya nyuklia cha Zaporizhzhia na moto ulioko katika eneo hilo kutokana na mashambulizi ya majeshi ya Russia.

Alieleza kuwa Ukraine imejaribu kushambulia miundombinu ya kiraia nchini Russia na “sisi hadi sasa tumejibu hilo kwa kujizuilia, lakini ni hivi sasa.”

“Iwapo hali itaendelea kwa muelekeo huu, tutajibu kwa nguvu zaidi,” Putin alisema.

“Hivi karibuni, majeshi ya ulinzi ya Russia yamefanya mashambulizi kadhaa yaliyosababisha athari kubwa,” alisema katika kile kinachoelekea kuonyesha mashambulizi ya Russia mapema wiki hii katika kinu cha nishati huko kaskazini ya Ukraine na bwawa lililoko kusini. “Tukadirie hayo kama ni mashambulizi ya kuonya.”

Waangalizi wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki likifanya tathmini ya uharibifu wa kinu cha nishati ya nyuklia cha Zaporizhzhia, Ukraine, Sept. 1, 2022.
Waangalizi wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki likifanya tathmini ya uharibifu wa kinu cha nishati ya nyuklia cha Zaporizhzhia, Ukraine, Sept. 1, 2022.

Amedai, bila ya kutoa maelezo halisi, kuwa Ukraine imejaribu kuanzisha mashambulizi “karibu na kituo cha nyuklia, vinu vya nishati ya nyuklia,” ikiongeza kuwa “tutalipiza kisasi iwapo wanashindwa kufahamu kuwa mbinu hizi hazikubali.

Russia imeripoti milipuko kadhaa na mashambulio katika miundombinu ya kiraia kwenye maeneo karibu na Ukraine, na pia katika bohari za silaha na vituo vingine. Ukraine imedai kuhusika katika baadhi ya mashambulizi hayo na imejizuia kueleza chochote kuhusu hayo mengine.

Rais Vladimir Putin (kulia) na Waziri Mkuu wa India Narendra Modi.
Rais Vladimir Putin (kulia) na Waziri Mkuu wa India Narendra Modi.

Putin pia amejaribu Ijumaa kuiondoa India wasiwasi kuhusu mgogoro wa Ukraine, akimwambia Waziri Mkuu wa India Narendra Modi kuwa Moscow inataka kuona vita vinamalizika haraka na akidai kuwa maafisa wa Ukraine hawataki kufanya mazungumzo.

“Najua msimamo wako kuhusu vita vya Ukraine na pia wasiwasi uliokuwa umerejea mara kadhaa kuuelezea,” kiongozi wa Russia alimwambia Modi.

“Tutafanya kila tunaloweza kumaliza kwa haraka iwezekanavyo. Bahati mbaya, upande wa pili, uongozi huo wa Ukraine, umekataa mchakato wa mazungumzo na kueleza kuwa inataka kufikia malengo yake kwa njia ya kijeshi, katika medani ya vita.”

XS
SM
MD
LG