Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 16, 2024 Local time: 19:56

Serikali ya Ukraine yagundua kaburi la halaiki lililozikwa miili 440


Oleg Kotenko, kamishna anayehusika na masuala ya watu wasiojulikana waliko katika mazingira maalum, anaangalia makaburi yasiyotambulika ya raia na wanajeshi wa Ukraine katika eneo lilotekwa na Ukraine huko Izium, Sept. 15, 2022.
Oleg Kotenko, kamishna anayehusika na masuala ya watu wasiojulikana waliko katika mazingira maalum, anaangalia makaburi yasiyotambulika ya raia na wanajeshi wa Ukraine katika eneo lilotekwa na Ukraine huko Izium, Sept. 15, 2022.

Kaburi la halaiki lililozikwa zaidi ya miili 440 limegunduliwa huko Izium, upande wa kaskazini mashariki ya Ukraine, ambapo wanajeshi ya Russia waliondolewa siku chache zilizopita, maafisa wa Ukraine walisema Alhamisi.

“Ninaweza kusema ni moja ya maeneo ya mazishi makubwa kabisa katika mji mkubwa katika maeneo [yaliyokombolewa] … miili 440 ilikuwa imezikwa sehemu moja, Serhiy Bolvinov, mkuu wa upelelezi wa jeshi la polisi katika mkoa wa Kharkiv, amekieleza kituo cha televisheni cha Sky News, kulingana na Reuters. “Baadhi walifariki kwa sababu ya kupigwa na makombora … wengine walifariki kwa sababu ya mashambulizi ya angani.”

Katika hatua ya Ukraine kujibu mashambulizi waliweza kuyasukuma wanajeshi wa Russia kutoka katika mkoa huo mwisho wa wiki iliyopita. Majeshi ya Russia yalikuwa yamefanya uvamizi wa jiji hilo katika mkoa wa Kharkiv. Maafisa wa Ukraine walisema wanajeshi hao waliacha nyuma kiwango kikubwa cha silaha na vifaa, Reuters imeripoti.

Reuters haikuweza kuthibitisha madai ya Ukraine, na hapakuwa na tamko la haraka kwa umma kutoka Russia kuhusu madai hayo.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy, ambaye alitembelea hivi karibuni jiji lililorejeshwa mikononi mwa Ukraine Jumatano, alisema Russia ndiyo ilihusika. Alifananisha kugunduliwa kwa miili huko Izium kuwa sawa na tukio la Bucha, kitongoji cha Kyiv, wakati uvamizi wa Russia ulivyoanza mwishoni mwa mwezi Februari.

“Russia imeacha miili kila mahali na lazima iwajibishwe,” Zelenskyy alisema katika hotuba yake kwa njia ya video Alhamisi jioni. Alisema atatoa taarifa zaidi kuhusu eneo la kaburi la halaiki huko Izium siku ya Ijumaa.

Ukraine na washirika wake wa Magharibi wameyashutumu majeshi ya Russia kwa kuendeleza vitendo vya uhalifu wa vita huko. Russia imekanusha kuwa inawalenga raia au kutenda uhalifu wa kivita.

Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa unakutana siku ya Ijumaa kutathmini hoja ambayo itamruhusu Zelenskyy kuzungumza katika Baraza hilo kuwa njia ya ujumbe wa video. Mwaka huu, UN inataka hotuba zote zitolewe na mtu mwenye akiwepo mkutanoni. Hata hivyo, idadi ya waliowengi ya wastani ya wanaohudhuria na kupiga kura ndiyo kinachohitajika kwa hoja hiyo kupita.

Rais wa Marekani Joe Biden alitangaza msaada mwengine wa silaha wenye thamani ya dola za Marekani milioni 600 kwa Ukraine, ikiwa ni mara ya 21 Wizara ya Ulinzi imetoa silaha na vifaa vingine na kuvifikisha Ukraine, White House imesema.

Habari hii inatokana na vyanzo mbalimbali vya habari ikiwemo Reuters, AFP, AP

XS
SM
MD
LG