Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 13:41

Rais wa China azuru Kazakhstan na Uzbekistan


Ziara ya Rais wa China Xi Jinping Kazakhstan. Rais wa Kazakh Kassym- Jomart Kemeluly Tokayev (kushoto) akiwa na Rais Xi.
Ziara ya Rais wa China Xi Jinping Kazakhstan. Rais wa Kazakh Kassym- Jomart Kemeluly Tokayev (kushoto) akiwa na Rais Xi.

Rais wa China Xi Jinping anatembelea Kazakhstan na Uzbekistan, nchi mbili ambazo zina idadi kubwa zaidi ya watu katika Asia ya Kati, katika ziara ambayo baadhi ya wataalam wanasema imelenga kuonyesha baadhi ya mafanikio ya juhudi za Mradi wa Barabara wa China, Belt and Road Initiative.

Ni ziara ya kwanza nje ya nchi kwa Xi tangu Shirika la Afya Duniani lilipotangaza mlipuko wa COVID-19 kama suala la dharura ya afya ya umma mwaka 2020.

Kuwasili kwake huko Kazakhstan Jumatano kumetokea mwezi moja kabla ya Mkutano wa Chama cha Kikomunisti cha China kufanyika huko Beijing ambao unafanyika kila baada ya miaka mitano. Xi anatarajiwa kuchaguliwa kwa mhula wa tatu, jambo ambalo halijawahi kufikiwa kama kiongozi wa nchi hiyo wakati wa mkutano wa mwaka huu.

Wakati akikutana na Rais wa Kazakh Kassym- Jomart Kemeluly Tokayev, Xi amesisitiza uungaji mkono wake wa kuheshimu mipaka na uhuru wa Kazakhstan.

“Haijalishi namna hali ya kimataifa itakavyobadilika, tutaendelea kuiunga mkono Kazakhstan kwa nguvu zote katika kulinda uhuru wake, utawala wake na mipaka yake, na pia kusaidia kikamilifu kwa mageuzi mnayoyafanya ili kuhakikisha utulivu na maendeleo, na kukataa kabisa kuingiliwa na majeshi yoyote kuamua masuala ya ndani ya nchi yenu,” Xi alisema katika taarifa iliyotolewa na Kazakhstan.

Xi alikuwa anatarajiwa kusaini nyaraka kadhaa za ushirikiano wa pande mbili na rais wa Kazakh, kulingana na wizara ya mambo ya nje ya Kazakh.

Akiwa mshiriki wa karibu wa pande zote Russia na China, iliyokuwa Jamhuri ya Soviet imeripotiwa kuwa inahisi vitisho zaidi kutokana na hatari zilizokuwepo kwa mipaka yake tangu vita vya Ukraine kuanza. Kazakhstan bado haijatatua kikamilifu mgogoro wa mipaka na jirani yake wa kaskazini, Russia.

Kulingana na Saparboy Jubayev, mchumi katika Chuo Kikuu cha Kitaifa cha Eurasian huko Kazakhstan, nchi hiyo tayari imekwisha tatua masuala ya mipaka na China na itafurahia uungwaji mkono kamili na Xi kwa ajili ya kujitawala wakati viongozi hao wawili wakikutana na Rais wa Russia Vladimir Putin baadae wiki hii huko Samarkand, Uzbekistan.

Viongozi wa India, Pakistan, Kyrgyzstan, Tajikistan, Kazakhstan na Uzbekistan pia wanahudhuria Mkutano wa viongozi wa Jumuiya ya Ushirikiano wa Shanghai Alhamisi na Ijumaa huko katika jiji la pili kwa ukubwa nchini Uzbekistan – ikiwa ni kituo muhimu katika Barabara ya asili ya Hariri inayounganisha China na Ulaya. Tangu ilipoanzishwa mwaka 2001, vipaumbele vya jumuiya ya SCO vimejumuisha usalama wa eneo na masuala ya maendeleo.

XS
SM
MD
LG