Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 07:46

Museveni, Besigye, Bobi na Muntu wajiandaa uchaguzi 2021 Uganda


Rais Museveni akimpa mkono hasimu wake wa kisiasa Besigye, kwa mara ya kwanza baada ya miaka 25
Rais Museveni akimpa mkono hasimu wake wa kisiasa Besigye, kwa mara ya kwanza baada ya miaka 25

Treni ya siasa za Uganda inakimbia kwa kasi zaidi kabla ya kuanza uchaguzi mkuu wa 2021.

Mahasimu wa kisiasa watakaorejea ulingoni tena katika kinyang’anyiro hicho cha kugombea urais akiwemo Rais aliyeko madarakani Yoweri Museveni na Kizza Besigye, wanaonekana kutumia fursa ya utamaduni uliyokuwepo dhidi ya wapinzani wao, wameanza kampeni zao katika matukio mawili tofauti kwa kupishana siku chache.

Hayo yamechambuliwa na gazeti la The East African, Jumapili, wakifafanua kuwa Rais Museveni, 74, ambaye atakuwa anagombea kwa awamu ya sita, amejiandaa kufikisha matakwa yake ya kuwepo katika utawala kwa kipindi cha miaka 40 ifikapo mwaka 2026.

Alipata kile kilichokuwa kinatarajiwa katika “ombi” lililotolewa na wanachama wa kamati kuu ya utendaji (CEC) ya chama tawala cha NRM, chombo cha juu kinachosimamia sera za chama, “ajitolee kuwania nafasi kama mgombea pekee” ifikapo 2021.

Rais Museveni aliwakusanya CEC katika hoteli ya kifahari ya Chobe Safari Lodge iliyoko karibu na Mto Nile wakati ombi hilo la kugombea tena lilipotolewa.

Kwa mujibu wa Mike Mukula, mmoja kati ya manaibu wenyeviti watano wa mikoa wa chama hicho, NRM “inachukuwa muelekeo huu kwamba mpaka pale ambapo Museveni atahisi, “Ni sawa, hivi sasa tumefika tunapotaka’ na kuamua kustaafu, ataendelea kuwa nahodha wetu.”

Dkt Besigye kwa upande wake ametangaza kile alichokiita “Baraza la Mawaziri la Wananchi” yeye mwenyewe akishikilia nafasi ya juu kama rais na kiongozi aliyeko madarakani wa chama chake cha Forum for Democratic Change Patrick Amuriat Oboi kumchagua kuingia katika baraza maalum aliloliita Baraza la Rais la Serikali. Baraza hilo litakuwa na mawaziri 37 na mawaziri chini ya ofisi ya rais.

Kwa kuendelea kushikilia nafasi hiyo ya juu, Dkt Besigye, 62, anajiandaa kupambana na hasimu wake wa kisiasa Rais Museveni kwa mara ya tano.

Marafiki hao wawili wa zamani wakati wakiwa katika vita vya msituni vya mtutu wa bunduki kati ya mwaka 1981 -86 harakati zilizomwezesha Rais Museveni kuingia madarakani, wamekuwa wakigombea katika kinyang’anyiro cha urais tangu mwaka 2001. Dkt Besigye alikuwa ni daktari wa Museveni wakati wako msituni.

Kuna wanasiasa wawili ambao kunauwezekano mkubwa kutoa changamoto katika uchaguzi unaokuja -- mwanamuziki na mwanasiasa Robert Sentamu Kyagulanyi aka Bobi Wine, 37, na Meja Jenerali wa jeshi wa zamani Mugisha Muntu, 60.

Bobi Wine hajaweka wazi kabisa hatma ya umashuhuri wake kisiasa kutoka jukwaa la muziki kufikia la kisiasa katika kipindi cha miaka miwili.

Akizungumza na kituo cha televisheni cha CNN Februari 2 alisema "anafikiria kwa uzito mkubwa" kugombea nafasi ya urais 2021. Wakati huo huo amesema kuwa hayuko peke yake katika mchakato huo, mpaka sasa hajatoa muundo mzima wa timu yake utakaopeleka mbele dira yake.

Mugisha Muntu aliondoka chama cha FDC kwa hasira na kutangaza kuwa jukwaa jipya The New Formation ni la watu wenye fikra zinazofanana na wale waliokuwa hawajafurahishwa na chama cha FDC.

Muntu na wenzake walisema kuwa wanajitoa kutoka chama hicho walichodai ni chenye mazingira hatarishi kinachoongozwa na watu wanaotiliwa mashaka na wasioaminika, hususan katika kipindi ambacho yeye alikuwa rais wa chama hicho.

XS
SM
MD
LG