Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 11:55

Museveni atishia kuwafukuza wawakilishi wa haki za binadamu


Rais Yoweri Museveni
Rais Yoweri Museveni

Rais wa Uganda Yoweri Museveni anataka nchi za nje kukoma kuingilia maswala ya ndani ya nchi yake akisema hatua hiyo ni ukosefu wa maadili na heshima.

Museveni, anataka watetezi hao wa haki za binadamu kuacha kumkosoa akitishia kuwafukuza Uganda.

Rais pia anataka mashirika ya kutetea haki za binadamu kukoma kukosoa utawala wake, akisema kama wanataka kazi ya kutetea haki za kibinadamu, waende nchi kama Somalia ambapo mfumo wake wa utawala sio thabiti.

Katika hotuba yake kwa taifa, Museveni alikosoa wito wa wapinzani wake na watetezi wa haki za kibinadamu, wanaotaka mataifa ya nje kusitisha msaada kwa Uganda, kutokana na madai ya dhulma dhidi ya wapinzani wake.

Wanasiasa wa upinzani, pamoja na mawakili wa mbunge Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobi Wine, wanataka Marekani kusitisha msaada wa kijeshi kwa Uganda wakisema utawala wa Museveni unatumia silaha hizo kuuwa raia wake, Jambo linaloungwa mkono na watetezi wa haki za kibiandamu.

"Hamkushiriki katika vita vilivyo komboa nchi hii. Sasa mpo hapa mnakula sumbusa kwa starehe zenu. Hawa vijana wakifanya makosa, ni jukumu langu kuwasaidia kwa sababu mimi ndio nimewakuza. Sio kazi yenu," ameeleza Museveni.

Museveni amesema kwamba hatakubali mataaifa ya nje kuingilia kati siasa za Uganda, akisisitiza kwamba wabunge Bobi Wine, Francis Zaake, hawakupigwa wanavyodai, akiongezea kwamba anasubiri uamuzi wa mahakama kabla ya kuwachukulia hatua kali wote wanoeneza habari anazoziita uvumi, za kupigwa Bobi Wine, ili wamlipe kwa kumchafulia jina.

Hotuba ya Museveni, inajiri baada ya aliyekuwa mkuu wa polisi Mohammed Kirumira, kuuawa kwa kupigwa risasi. Kirumira, amekuwa akisema hadharani kwamba maafisa wa ngazi ya juu katika polisi, ndio wanaoshirikiana na makundi ya wahalifu kuua na kutesa rais wakiwemo maafisa wengine maarufu nchini Uganda.

Kabla ya kuawa, Kirumira alifikiswa mbele ya kamati ya nidhamu ya polisi na kufunguliwa mashtaka ya ulaghai, kuwatesa watu, mauaji miongoni mwa mengine, ambayo yalifutiliwa mbali baadaye kwa ukosefu wa ushahidi, lakini akasisitiza kwamba jeshi la polisi la Uganda linaongozwa na wahalifu.

XS
SM
MD
LG