Pendekezo hili lililowasilishwa na wakuu wa SAA kwa chama cha wafanyakazi wiki hii ambalo halijaidhinishwa na wafanyakazi ni ishara nyingine kwamba shirika hilo linalomilikiwa na taifa liko ukingoni wa kuvunjika.
Mazungumzo na vyama vya wafanyakazi yataendelea tena Jumatatu kulingana na hati ambazo shirika la habari la reuters limepokea.
SAA, shirika kubwa la ndege la Afrika liliingia katika mpango wa kujilinda kutokana na hali ya kufilisika mwezi Disemba 2019, na tangu wakati huo lililazimika kusitisha safari zake zote za abiria kutokana na janga la virusi vya korona kote duniani.
Wiki hii maafisa wa serikali wamewaambia wakuu wa shirika hilo kwamba hawatatoa fedha zaidi, wala kudhamini mipango ya mikopo au kuruhusu mpango wa kunusuru shirika kutokana na fedha zinazotoka nje.
Kulingana na mpango wa malipo ya uzeeni wafanyakazi hao ajira zao zitasitishwa kwa makubaliano yatakayo fikiwa na pande zote hapo April 30.
Watakuwa na haki yakulipwa mshahara wa wiki moja kwa kila mwaka waliofanyakazi, kulipwa mwezi mmoja badala ya malipo ya kusitishwa kazi na kulipwa siku za likizo zao zilizobaki.
Msemaji wa SAA amekataa kutoa matamshi yoyote juu ya pendekezo hilo huku vyama viwili vya wafanyakazi vikithibitisha kwamba pendekezo hilo limewaslishwa na watajadili na wanachama wao.
Imetayarishwa na Mwandishi wetu, Abdushakur Aboud, Washington, DC