Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 23:04

Afrika Kusini yarekodi vifo 5 kwa siku moja kutokana na Corona


Ilani ya kuwataka watu wakae nyumbani Afrika Kusini
Ilani ya kuwataka watu wakae nyumbani Afrika Kusini

Afrika Kusini imerekodi vifo vya watu watano kwa siku moja kutokana na virusi vya Corona. Idadi hiyo ndiyo ya juu zaidi kuwahi kuripotiwa katika nchi hiyo ndani ya siku moja.

Kufikia Alhamisi, jumla ya watu 18 walikuwa wamepoteza maisha yao kutokana na maambukizi ya Corona katika taifa hilo.

Nchini Somalia, wizara ya afya imesema mtu mmoja, mwanamme mwenye umri wa miaka 58, amekufa kutokana na maambukizi ya Corona.

Mtu huyo hana historia yoyote ya kusafiri nje ya Somalia na alikuwa akipata matibabu katika hospitali ya Martini kwenye mji mkuu wa Mogadishu.

Uganda imepiga marufuku watu kufanya mazoezi nje ya nyumba zao kama hatua ya kudhibithi maambukizi ya Corona.

Rais Yoweri Museveni ameamrisha watu wanaotaka kufanya mazoezi kufanya hivyo nyumbani. Baadaye video na picha zilizomuonyesha akifanya mazoezi ndani ya nyumba zilienea mitandaoni.

Museveni ametoa amri hiyo baada ya video na picha zinazoonyesha watu wakifanya mazoezi barabarani jijini Kampala, kusambaa kwenye mitandao ya kijamii.

Nchini Kenya wabunge wamelazimika kuweka wazi matokeo ya vipimo vya Corona walivyofanyiwa baada ya vyombo vya habari nchini humo kuripoti kwamba baadhi ya wabunge walikuwa wameambukizwa virusi hivyo na kuzua wasiwasi mkubwa kati ya raia ambao hutangamana nao kila siku.

Maabara ya Lancet, walikofanyiwa vipimo wabunge, imekanusha ripoti hizo za vyombo vya habari vya Kenya, ikisema ni za uongo na za kupotosha.

Lancet imetaka vyombo vya habari vya Daily Nation na The Star, vilivyochapisha habari hiyo kuomba msamaha.

-Imetayarishwa na Kennes Bwire, VOA, Washington DC

XS
SM
MD
LG