Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumatatu, Mei 06, 2024 Local time: 20:48

Maandamano yaanza tena Nairobi


Maafisa wa polisi wa Kenya wakiondoa vizuizi kwenye barabara kuu huko Kibera jijini Nairobi tarehe 2 Mei, 2023. Picha na Luis Tato / AFP.
Maafisa wa polisi wa Kenya wakiondoa vizuizi kwenye barabara kuu huko Kibera jijini Nairobi tarehe 2 Mei, 2023. Picha na Luis Tato / AFP.

Maafisa wa polisi wa kutuliza ghasia nchini Kenya, walisambaa katika mji mkuu wa Nairobi siku ya Jumanne asubuhi kuthibiti maandamano yaliyo andaliwa na viongozi wa upinzani.

Katika maandamano hayo wanaodai haki ya uchaguzi, wakiulaumu utawala mbovu wa rais William Ruto na kupanda kwa gharama za maisha baada ya mazungumzo na wabunge wa pande mbili kusambaratika.

Polisi wamelazimika kufunga barabara zote zinazoelekea mji mkuu wa Nairobi, wengi wa maafisa hao wakiwa wamezagaa katika barabara inayoelekea Ikulu, ofisi za serikali, barabara ya Ngong, barabara ya Landhies, Kenyatta, barabara kuu ya Uhuru, mzunguko wa Bunyala, barabara ya Mombasa karibu na mzunguko uliopo katika eneo la Imara Daima, na barabara nyingine zinazoelekea katikati ya jiji.

Siku nzima ya Jumanne jiji kuu la Kenya lilishuhudia uwepo mkubwa wa polisi katika mitaa ya Mathare na Kibra, kuwatawanya waandamanaji waliokuwa wamejitokeza kushiriki katika maandamano ambayo serikali imeyatangaza yameharamishwa.

Maafisa wa kikosi cha kutuliza ghasia walitumia mkakati wa kuvaa nguo za kiraia ili kupambana na waandamanaji waliotishia kukiuka agizo la serikali na kuingia mjini.

Hata hivyo duru mpya ya maandamano ya upinzani yalitanguliwa na matukio mawili tofauti ya uchomaji magari, gari la abiria kwenye barabara ya Ngong na lori la mizigo lililokuwa likisafirisha nyanya za umeme kuelekea Kampala Uganda kutoka Mombasa. Upinzani umekana kuhusika na matukio hayo.

Awali, msafara wa wabunge wa upinzani uliokusudia kuwasilisha hati za matakwa yao kwenye ofisi ya rais iliyopo kwenye barabara ya Harambee katikati ya jiji, ulisambaratishwa na mabomu ya kutoa machozi, na kuzuiliwa kuingia katikati ya jiji hilo.

Maandamano mapya dhidi ya serikali, yanafuatia kusambaratika kwa majadiliano kati ya serikali na upinzani, pamoja na kwamba kamati ya teule iliundwa na kuweka hadidu za rejea na mchakato wa majadiliano.

KENNEDY WANDERA, SAUTI YA AMERIKA, NAIROBI.

XS
SM
MD
LG