Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 02:38

Jumuiya za haki za binadamu na raia zaitaka UN kushughulikia mgogoro unaofukuta Tanzania


Dkt Abbas Maelezo
Dkt Abbas Maelezo

Jumuiya 38 zinazo simamia haki za binadamu na raia ulimwenguni zinataka serikali ya Tanzania kushughulikia hali inayozidi kuwa mbaya ya ukandamizaji wa haki za binadamu inayoendelea nchini humo.

Gazeti la The East African limeripoti Jumamosi kuwa katika barua ya wazi iliyotumwa mwisho mwa wiki hii kwa Wawakilishi Wakazi wa Kudumu wa Wanachama na Waangalizi wa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, taasisi hizo zinataka hatua zichukuliwe dhidi ya serikali ya Tanzania wakati wa Kikao cha 41 cha Baraza hilo kilichopangwa kufanyika kati ya Juni 21 na Julai 12.

“Wakati hatuamini kuwa katika hatua hii, hali hiyo inahitaji kupitishwa azimio, kuna dalili zote za kututahadharisha kuwa mgogoro wa kuminywa kwa haki za binadamu unafukuta,” imesema barua hiyo, ambayo imesainiwa na Mtandao wa kutetea haki za binadamu wa Bara la Afrika, Shirika la Amnesty International, Shirika la ARTICLE 19, Shirika la Asian Forum for Human Rights and Development, Kituo cha Centre for Civil Liberties – Ukraine, Human Rights Watch na Tume ya International Commission of Jurists na taasisi nyingine.

Jumuiya hizo zimesema kuwa tangu asasi za kiraia 30 zilipotuma barua juu ya hali ya Tanzania kwa Waangalizi na Wanachama wa Baraza Agosti 2018, uhuru wa wanaotetea haki za binadamu, jumuiya za kiraia, waandishi wa habari, wenye blogi, vyombo vya habari, mashoga na upinzani na wale wenye maoni tofauti na serikali umeendelea kudidimia.

Lakini, msemaji wa serikali Dkt Hassan Abbas, amesema kuwa Tanzania tayari ilikuwa imeshakabidhi ripoti yake ya haki za binadamu mapema mwaka huu kwa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa na mpaka sasa haijapokea barua yoyote kutoka UN juu ya malalamiko ya unyongeshwaji wa haki za binadamu.

“Tunajua kuwa kuna baadhi ya asasi za kiraia ambazo zinatumiwa na mataifa yenye nguvu ambazo zimepeleka malalamiko UN juu ya hali ya haki za binadamu Tanzania. Lakini ripoti tuliokabidhi UN itakuwa ni msimamo wa serikali juu ya suala lolote litakalo ibuka juu ya haki za binadamu,” amesema Dkt Abbas ambaye aliongeza kusema kuwa serikali haiwajibiki kwa asasi za kiraia ambazo zinafanya propaganda zisizokuwa na msingi wowote.

XS
SM
MD
LG