Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 08:15

Afrika Mashariki yakabiliwa na mafuriko makubwa yasiotabirika


Hali ilivyokuwa katika eneo la Jangwani mjini Dar es Salaam baada ya mvua kubwa kunyesha Jumanne, Oktoba 13, 2020. Picha kwa hisani ya Global Publishers TV, Tanzania.
Hali ilivyokuwa katika eneo la Jangwani mjini Dar es Salaam baada ya mvua kubwa kunyesha Jumanne, Oktoba 13, 2020. Picha kwa hisani ya Global Publishers TV, Tanzania.

Katika miezi ya karibu, mafuriko makubwa ambayo hayatabiriki yameosha sehemu nyingi za Kenya, Sudan, Ethiopia na nchi kadhaa za Afrika Mashariki na Kati na kuharibu nyumba na maisha kwa wakati mmoja.

Wakati huohuo serikali zinaendelea kuijitahidi kupambana na janga la COVID-19 ulimwenguni. Uganda ni moja ya nchi ambazo zimeathiriwa vibaya na mafuriko haya.

Wakati dunia ikipambana na janga hilo, sehemu kubwa katika bara la Afrika limefunikwa na mafuriko. Hali hii iko kote mashariki mwa Uganda katika mji wa Jinja, na kwenye fukwe za Ziwa Victoria.

Tangu mwezi Machi, mafuriko yamesababisha watu 400 kupoteza maisha huko Afrika Mashariki.

Nchini Uganda, shirika la Catholic Relief Services linakadiria kwamba kiasi cha watu 580,000 wameathiriwa, kuanzia kwenye nyumba zilizoko pembezoni mwa ziwa mjini Kampala hadi kwenye mashamba madogo kwenye mpaka wa Kenya.

Niek de Goeij, wa Catholic Relief Services anasema, “wewe ni mkulima mdogo ambaye kwa kawaida unanufaika na kilimo cha kwenye ukingo wa mto. Ghafla kuna mafuriko makubwa yanatokea mlimani kwa sababu ya mvua nyingi zinazonyesha, unajua, unapoteza kila kitu.”

Katika mji wa Jinja, mtangazaji wa radio na mwanaharakati wa mazingira, John Hillary anasema mafuriko siyo tu yanaharibu nyumba – yanaharibu mfumo mzima wa kuiweka jamii pamoja.

“Hospitali pekee ya umma katika mkoa wa Chilembwe, iliharibiwa kabisa. Kwa sababu ya mafuriko watu wameugua. Lakini hawakuweza kwenda popote kwa sababu hospitali imeharibiwa,” Hillary anasema.

De Geoij anasema mvua kubwa ni jambo la kawaida Afrika Mashariki. Kisicho cha kawaida, ni mvua za mara kwa mara na zisizo na uhakika. Anasema Uganda inakabiliwa na tisho mara tatu ambalo linafanya iwe ni vigumu sana kwa makundi kusaidia.

“Tuna nzige, tuna mafuriko. Na halafu, juu ya yote hayo, tuna COVID-19. Na watu wameathiriwa sana, umekuwa ni mwaka mgumu sana, unafahamu, kufungiwa shughuli na kuathiriwa na mafuriko, na halafu kwa sababu ya kufungwa huko, fursa ya kupata misaada na ile inayostahili inakuwa ngumu kidogo,” Goeij anasema.

Hillary, ambaye ni mtangazaji wa radio, anazungumza mara kwa mara kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa. Alikulia shamba, hili kwake ni jambo la binafsi sana.

“Kadri muda unavyokwenda, tumegundua kwamba, kwa sababu ya uzembe, tumekuwa tukijihusisha na taratibu ambazo zimeharibu kabisa mzunguko wetu wa mvua, hali yetu ya hewa imezidi kuwa mbaya kila siku. Nina miaka 26 tu, nimeona kadri muda unavyokwenda dunia yangu inazidi kuwa mbaya. Sitaki kuona hilo linawatokea watoto wangu.” Hillary anasema.

Hili anasema ni jinamizi la maisha. Hapa ni nyumbani, na anataka vizazi vijavyo kuuona uzuri huu pia.

XS
SM
MD
LG