Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 04, 2024 Local time: 02:51

Viongozi wa Afrika Mashariki watoa wito mpya wa kusitishwa mapigano DRC


Maafisa wa Jeshi la DRC wakiwa katika eneo la tukio la shambulizi.
Maafisa wa Jeshi la DRC wakiwa katika eneo la tukio la shambulizi.

Viongozi wa kanda ya Afrika Mashariki Jumamosi walitoa wito mwingine mpya wa kusitishwa mara moja kwa mapigano na pande zote katika mzozo wa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambao unahusisha jeshi la nchi hiyo dhidi ya  kundi la waasi ambalo limeishutumu Rwanda kwa kuliunga mkono.

Katika mkutano wa viongozi uliofanyika katika mji mkuu wa Burundi Bujumbura, viongozi wa jumuiya ya kikanda ya Afrika Mashariki walitaka kusitishwa mara moja kwa mapigano na pande zote, kulingana na taarifa iliyotolewa mwishoni mwa mkutano huo.

Kundi la waasi la M23 limeteka sehemu kubwa ya jimbo la Kivu Kaskazini mashariki mwa Congo katika mashambulizi ya haraka tangu Oktoba 20 ambayo yameutishia mji mkuu wa jimbo hilo, Goma.

Mzozo huo umezidisha mivutano ya kikanda huku Congo ikimshutumu jirani yake Rwanda kwa kuunga mkono na kufadhili uasi unaoongozwa na Watutsi. Wataalamu wa Umoja wa Mataifa na mataifa ya Magharibi pia wameishutumu Rwanda kwa kuliunga mkono kundi la M23, ingawa Rwanda imekanusha kuhusika kwa vyovyote vile.

Mkutano wa Jumamosi ulikuwa juhudi za hivi punde zaidi za kidiplomasia za kujaribu kumaliza uasi huo, ambao umewakosesha makazi takriban watu 520,000 tangu Machi 2022 huko Kivu Kaskazini, eneo ambalo limekumbwa na migogoro kwa muda mrefu.

Mapema wiki hii, Papa Francis alizuru Congo na kutoa wito wa kukomeshwa kwa ghasia.

Viongozi wa kanda walikuwa wamepitisha makubaliano mwezi Novemba ambapo waasi walitarajiwa kusitisha mapigano na kujiondoa kwenye maeneo yaliyochukuliwa hivi karibuni ifikapo Januari 15, lakini hilo halikufanyika.

Ripoti ya ndani ya Umoja wa Mataifa ilisema waasi hao walikuwa wakikiuka masharti ya sitisho la mapigano na kujiondoa.

Mkutano huo wa Jumamosi ulihudhuriwa na wakuu wa nchi kutoka Rwanda, Congo, Uganda, Kenya, Tanzania na Burundi na maafisa wakuu kutoka kanda hiyo.

Pia wametaka makundi yote ya kigeni na yenye silaha yaondoke kutoka Congo na kuwataka wakuu wa kijeshi wa Kanda kukutana ndani ya wiki moja na kuweka muda wa kuondoka.

"Mkutano huo ulirudia kusisitiza wito wake kwa pande zote kupunguza kusambaa kwa mivutano," taarifa hiyo ilisema.

Januari 27, waasi wa M23 walichukua udhibiti wa mji wa Kitshanga katika eneo la Masisi na kudhibiti barabara mpya, na kuutenga zaidi mji mkuu wa jimbo la Goma.

XS
SM
MD
LG