Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 06:47

Upungufu wa Chakula: Baraza la nafaka la EAC lakutana Arusha


Mkulima katika Kwale, nchini Kenya.
Mkulima katika Kwale, nchini Kenya.

Wajumbe wa baraza lanafaka la nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamekutana Alhamisi jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania kujadili namna ya kukabiliana na tatizo la ukame.

Ukubwa wa tatizo

Tatizo hilo tayari limezikumba nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na kusababisha uhaba wa chakula kwa baadhi ya wananchi na pia kuendelea kuwepo kwa mfumuko wa bei za mazao ya nafaka.

Mwandishi wa idhaa ya Kiswahili VOA ameripoti kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la nafaka la nchi za ukanda wa Afrika Mashariki, Gerald Masila amesema kikao hicho ambacho kinashirikisha wadau wa sekta za kilimo kutoka nchi zote wananchama wa Jumuiya ya Afrika mashariki wakiwemo watafiti.

Kikao hiki kinalenga kuweka mfumo mmoja wa kuziwezesha nchi wanachama kusaidiana katika kukabiliana na tishio hilo la uhaba wa chakula linalowakabili wananchi.

Wadau wahamasishwa

Aidha Gerald Masila amesema wakati wanaendelea na hatua hiyo pia wameanza kuhamasisha wadau wa kilimo wa nchi hizo kuwaelimisha wananchi wao kuondokana na dhana iliyojengeka kuwa chakula ni mahindi pekee na waanze kutumia aina nyingine ya vyakula.

Naibu katibu mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeshughulikia sekta ya huduma na uzalishaji Christopher Bazivamo amesema hatua ya kuwakutanisha wadau hao ni miongoni mwa jitihada zinazolenga kupata ufumbuzi wa pamoja wa tatizo hilo.

Mfumuko wa bei

Malalamiko ya wananchi juu ya kupanda kwa bei ya vyakula vya nafaka katika nchi mbalimbali za Jumuiya ya Afrika Mashariki yamekuwa yakiongezeka siku hadi siku,

Hata hivyo baadhi ya wanawake wa Jiji la Arusha nchini Tanzania wamesema kwa sasa wamelazimika kuanza kubadili aina ya vyakula na kuzizoesha familia zao kula vyakula vingine vikiwemo viazi na mihogo japo pia wamesema vimeanza kupanda bei.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo wa Baraza la nafaka katika nchi Jumuiya ya Afrika Mashariki mfumuko wa bei untofautiana kulingana na nchi ambapo nichini Tanzania imefikia asilimia 40 ikifuatiwa na Rwanda ambayo ni asilimia 28.

XS
SM
MD
LG