Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:42

Ujerumani kumuaga Chansela Merkel aliyeongoza kwa miaka 16


Chansela Angela Merkel (Markus Schreiber/Pool via Reuters)
Chansela Angela Merkel (Markus Schreiber/Pool via Reuters)

Ujerumani inafanya maandalizi ya kumuaga Chansela Angela Merkel, ambaye anaachia madaraka baada ya uchaguzi uliopangwa kufanyika Jumapili.

Merkel ameongoza taifa hilo lenye uchumi mkubwa kuliko yote Ulaya kwa miaka 16 na amehusika katika maamuzi makubwa Ulaya na katika uwanja wa dunia.

Merkel alikuwa Chansela wa kwanza mwanamke na kiongozi wa kwanza aliyelelewa katika nchi iliyokuwa Ujerumani Mashariki.

Aliingia katika siasa wakati Pazia la Chuma lilipoporomoka huko Ulaya. Baada ya Ujerumani kuungana mwaka 1990, aliteuliwa kuwa waziri wa wanawake na vijana na mlezi wake, Chansela wa zamani Helmut Kohl..

Vyombo vya habari vya Ujerumani vilimpa jina la ‘binti yake Kohl’ – lakini haraka aliondoka katika kivuli cha mlezi wake na akawa kiongozi wa chama cha Christian Democrats (CDU) mwaka 2000. Kwa kura chache alishinda uchaguzi wa mwaka 2005 na kuongoza serikali ya mseto ya chama cha Christian Democrats na Social Democrats.

File : Oct. 1, 2010 Chansela Angela Merkel, kulia, na Chansela wa zamani Helmut Kohl
File : Oct. 1, 2010 Chansela Angela Merkel, kulia, na Chansela wa zamani Helmut Kohl

Alikabiliwa na mgogoro wake wa kwanza mkubwa miaka mitatu baadae kufuatia kuanguka kwa uchumi ulimwenguni. Hilo likitokea katika benki za Ujerumani, Merkel alifanikiwa kudhibiti hali hiyo. Akisimama pembeni ya waziri wake wa fedha Oktoba 2008, aliwaambia Wajerumani kuwa serikali itawalinda. “Tunawaambia wale wenye akiba zao benki kuwa ziko salama na Serikali ya Ujerumani itasimama imara kuzilinda.”

Mgogoro wa mabenki ulibadilika na kuwa mgogoro wa deni la sarafu ya euro. Merkel hakutaka kufuta deni hilo katika ukanda wa Ulaya. Akawa ni kiongozi aliyechukiwa na Ugiriki, ambayo ilibidi itekeleze sera kubwa sana ya kupunguza matumizi ili iweze kubakia katika matumizi ya sarafu ya euro. Ulaya iliyumba lakini euro ilinusurika.

“Ulaya inafeli pale euro inapofeli,” Merkel alisema mwaka 2012. “Ulaya inashinda wakati sarafu ya euro inaposhinda. Sarafu ya euro inashinda iwapo tunajenga umoja imara unaostahili jina hilo kwa sababu inaungwa mkono na misingi imara ya ushirikiano, ukuaji na mshikamano.”

“Merkel anajulikana kama ‘chansela wa mgogoro’,” Nico Friedl, mwandishi wa bunge wa gazeti la Suddeutsche Zeitung, ambaye amekuwa akifuatilia kazi za Merkel kwa miongo miwili, amesema.

“Alilazimika kutatua migogoro kadhaa ulimwenguni wakati akiwa madarakani, siyo tu kwa Ujerumani, lakini pia ndani ya Umoja wa Ulaya, na washirika wengine wa eneo la Altantic pia China na Russia,”amesema.

XS
SM
MD
LG