Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 09:59

Upinzani Somalia wadai Rais Farmajo ni kipingamizi


Rais Mohamed Abdullahi Farmajo
Rais Mohamed Abdullahi Farmajo

Rais Mohamed Abdullahi Farmajo wa Somalia ameitisha mkutano na viongozi wa majimbo matano ya nchi yake ili kujadili mzozo ulojitokeza wa kutayarisha uchaguzi wa rais na bunge baada ya muda wa muhula wake wa kwanza kumalizika Jumatatu usiku.

Taarifa hiyo imetolewa siku moja baada ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwataka viongozi wa Somalia kurudi mara moja kwenye mazungumzo ya kutayarisha uchaguzi, wakati taifa hilo likizidi kukabiliwa na mashambulio kutoka kundi la Al Shabab.

Wakati huohuo wachambuzi wanasema mzozo huu wa kisiasa unaweza kurudisha nyuma maendeleo yaliyopatikana nchini humo.

Shambulizi la kigaidi katika Afrik Hotel Mogadishu, Somalia, Feb. 1, 2021. Al-Shabab claimed responsibility for the deadly assault.
Shambulizi la kigaidi katika Afrik Hotel Mogadishu, Somalia, Feb. 1, 2021. Al-Shabab claimed responsibility for the deadly assault.

Rais Abdullahi Farmajo alishindwa kufikia makubaliano na marais wa majimbo matano yenye utawala wa ndani ya Somalia kabla muda wa muhula wake wa miaka minne kumalizika, juu ya namna ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu.

Kutofikiwa makubaliano kunazusha wasiwasi mkubwa wa Somalia kurudi kwenye malumbano ya kisiasa yaliyoweza kutanzuliwa kwa sehemu kubwa mnamo miaka 20 ya kujarbu kujenga demokrasia nchini humo. Na hali hii inaweza kuwapatia nguvu wapiganaji wa Al Shabab, kuendelea na mashambulizi yao ya kuvuruga usalama wa taifa hilo.

Hata hivyo kulingana na sheria iliyopitishwa na bunge mwaka 2020 rais na wabunge wanaweza kuendelea na mamlaka hadi uchaguzi mpya ufanyike ikiwa hali kama hii ya kisiasa inajitokeza

Lakini mvutano huo umesababisha muungano wa upinzani wa kisiasa na viongozi wa majimbo mawili kati ya matano kutangaza kutomtambua tena Farmajo kama Rais.

Abdirahman Abdishakur Warsame ni mmoja kati ya wanaotaka kugombania kiti hicho cha urais kwenye mungano huo wa upinzani na anasema hawatakubali juhudi zozote za kuongeza muda wa Farmajo na kwamba lazima aondoke.

Abdirahman Abdishakur Warsame, Mgombea kiti cha rais wa Somalia ameeleza : "Muda wa muhula wake umemalizika na yeye sio tu ni kipingamizi kwa taifa bali pia katika kutayarisha uchaguzi wa kitaifa. Hakuweza kufikia makubaliano na viongozi wa majimbo juu ya uchaguzi ujao kwa sababu aliondoka mkutanoni hawezi tena kushikilia wadhifa huo.

Muungano huo wa upinzani wenye pia marais wawili wa zamani unatoa wito wa kuundwa baraza la mpito la utawala wa kitaifa litakalo kuwa na spika wa bunge, viongozi wa upinzani na majimbo pamoja na wawkilishi wa mashirika ya kiraia ili kuongoza taifa hadi kufanyike uchaguzi.

Akilihutubia bunge siku ya Jumamosi Rais Farmajo anaegombania muhula wa pili amewatuhumu marais Ahmed Madobe wa jimbo la Jubaland na Said Abdullahi Dani wa Puntland kwa kukataa kufikia maridhiano na kubadili msimamo wao kutokana na makubaliano ya awali ya Septemba. Na kuongeza kulaumu kuwepo na ushawishi kutoka nje katika uchaguzi ujao.

Mohamed Abdullahi Farmajo, Rais wa somalia amelalamika kwa kusema : "Kwa hakika nina kuambieni kuna uingiliaji kati wa kigeni katika utaratibu wa uchaguzi wa taifa wa Somalia kwa jumla. Nilikuwa na matumaini tungeliweza kufanya kazi pamoja lakini hilo limeshindikana.

Rais Madobe anaeungwa mkono na Kenya anadai kwamba Farmajo anataka kuingilia kati utaratibu wa uchaguzi ndani ya jimbo lake. Kulikuwa na matumaini kwamba utawala wa Farmajo utaweza kupanga na kutayarisha uchaguzi wa kitaifa ili wananchi wote washiriki lakini umeshindwa kupanua utawala na ushawishi wake katika taifa zima ukiendelea kudhibiti mji mkuu wa Mogadishu pekee yake.

Hassan Mudane Mhadhiri katika chuo kikuu cha Somalia anasema hali ni nzito.

Mhadhiri huyo anaeleza : "Kuna hali ya kukata tamaa kutokana na hali liyoko hvi sasa. Wakiendelea namna hii basi itarudisha nyuma maendeleo na matumaini yaliyopaikana mnamo miaka 20 iliyopita."

Kulingana na makubaliano ya Septemba uchaguzi usio wa moja kwa moja ulipangwa ufanyika ambapo kwa mara nyingine tena baraza la wazee wa ukoordineret litawachagua wabunge na hapo wabunge kumchagua rais.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani Ned Price, alisema kwamba Marekani imesikitishwa na mvutano huo, na Washington ingelipendelea kwa viongozi wa nchi hiyo kuweka kando maslahi yao ya kisiasa na kufanya kazi kwa maslahi ya Wasomali wote, na kutanzua mzozo huo mara moja.

XS
SM
MD
LG