Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 13:43

Selma: Rais Biden aahidi kufikia lengo la demokrasia, ahudhuria kumbukumbu ya tukio la 'Jumapili ya Umwagaji Damu'


Rais wa Marekani Biden ashiriki katika kumbukumbu ya matembezi ya haki za kiraia kuvuka Daraja la Edmund Pettus huko Selma, Alabama.
Rais wa Marekani Biden ashiriki katika kumbukumbu ya matembezi ya haki za kiraia kuvuka Daraja la Edmund Pettus huko Selma, Alabama.

Rais Joe Biden alitumia kumbukumbu kali za tukio la “Jumapili ya Umwagaji Damu” huko Selma kuahidi tena kufikia lengo la demokrasia, na kulienzi tukio hilo lenye mafundisho linalotokana na harakati za haki za kiraia.

Hili limejiri wakati ambapo Rais Biden ameshindwa kuskuma kuimarishwa kwa ulinzi wa upigaji kura kupitia bunge na Mahakama ya Juu yenye waconservative wengi imekuwa ikikandamiza sheria muhimu ya upigaji kura.

“Selma ni tegemeo kubwa. Haki hiyo ya kupiga kura … kura yako ihesabiwe ni hatua muhimu ya demokrasia na uhuru. Kwa hilo kila kitu kinawezekana,” Biden aliuambia mkusanyiko wa watu zaidi ya 1,000 waliokuwa wameketi upande mmoja wa Daraja la kihistoria la Edmund Pettus, lililopewa jina la kiongozi anayejulikana Ku Klux Klan.

“Haki hii ya msingi inaendelea kushambuliwa. Mahakama ya Juu ya kiconservative imekwamisha Sheria ya Haki ya Kupiga Kura kwa miaka kadhaa. Tangu uchaguzi wa mwaka 2020, wimbi la majimbo na darzeni na darzeni za sheria dhidi ya upigaji kura zimechochewa na ‘Uongo Mkubwa’ na wanaokanusha uchaguzi ambao wamechaguliwa katika madaraka,” alisema.

Kama mgombea mwaka 2020, Biden aliahidi kufuatilia mabadiliko ya sheria kuimarisha kulinda haki ya kupiga kura.

John Lewis
John Lewis

Miaka miwili iliyopita, sheria yake ya 2021, iliyopewa jina la kiongozi wa haki za kiraia John Lewis, marehemu mwakilishi wa Baraza la Wawakilishi wa Georgia, ilijumuisha vifungu vinavyozuia mgawanyo wa upande mmoja wa chama wa wilaya za kibunge, kuondoa vikwazo vya kupiga kura na kuleta uwazi katika mfumo wa ufadhili wa kampeni ambao unaruhusu wafadhili matajiri kuchangia kwa siri shughuli za kisiasa.

Ilipitishwa na Baraza la Wawakilishi lililokuwa linadhibitiwa na Wademokrat, lakini ilishindwa kupata kura 60 zinazohitajika kuipeleka katika Baraza la Seneti hata lililokuwa chini ya udhibiti wa chama cha Biden. Hivi sasa Warepublikan wanaudhibiti wa Baraza la Wawakilishi, kupitisha sheria kama hiyo siyo rahisi kufanikiwa.

“Tunajua ni lazima tupate kura za Baraza la Wawakilishi,” Biden alisema, lakini inaelekea hakuna njia ya kufikia hili hivi sasa.

Ziara hiyo ya Selma ilikuwa ni fursa kwa Biden kuzungumza moja kwa moja na kizazi cha hivi sasa cha wanaharakati wa haki za kiraia. Wengi wao wanahisi wameangushwa kutokana na kukosekana upigaji hatua wa haki za kupiga kura na wanashauku kuona utawala wake unaendeleza suala hilo.

Ni matukio machache yamekuwa na kumbukumbu muhimu kwa harakati za haki za kiraia kama kilichotokea Machi 7, 1965, huko Selma na wiki kadhaa zilizofuatia.

Chanzo cha ripoti hii ni shirika la habari la AP

XS
SM
MD
LG