Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 09:27

Mwaka 2022 ulikuwa mbaya zaidi kwa Somalia, asema Guterres


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, Jumatano amesema mwaka 2022 ulikuwa mbaya zaidi kwa raia wa Somalia tangu 2017, kwa kiasi kikubwa kwa sababu ya ongezeko la mashambulizi kutoka kwa kundi la wanajihadi la Al-Shabaab, yaliyosababisha vifo. 

Taifa la Pembe ya Afrika ambalo limekumbwa na machafuko na pia linakabiliwa na ukame mbaya, limeshuhudia kuongezeka kwa mashambulizi huku vikosi vya serikali na wanamgambo washirika wakiendesha operesheni kukabiliana na wanamgambo wenye uhusiano na Al-Qaeda.

Guterres katika ripoti yake kwa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa amesema mashambulio yanayoendelea kufanywa na Al-Shabaab, yamesababisha ukiukwaji wa haki za binadamu, unyanyasaji wa kingono na ongezeko kubwa la vifo vya raia.

Katika kipindi cha kuanzia mwishoni mwa Agosti 2022 hadi mwanzoni mwa Februari 2023, amesema tume ya Umoja wa Mataifa kwa Somalia imerekodi ongezeko la asilimia 153 la vifo vya raia kufikia 1,059, pamoja na vifo 382, Al Shabab ikilaumiwa kwa vingi vya vifo hivyo.

Katika miezi ya hivi karibuni, jeshi la Somalia na wanamgambo wa koo wametwaa tena sehemu kadhaa za maeneo kutoka kwa Al-Shabaab katika operesheni iliyoungwa mkono na mashambulizi ya anga ya Marekani na kikosi cha Umoja wa Afrika.

Licha ya hayo kundi hilo bado linadhibiti sehemu za mbalimbali na linaendelea kufanya mashambulizi ya kulipiza kisasi.

Katika shambulio baya zaidi tangu mashambulizi ya serikali kuanzishwa mwaka jana, watu 121 waliuawa katika milipuko miwili ya mabomu yaliyotegwa kwenye gari katika wizara ya elimu mjini Mogadishu mwezi Oktoba.

XS
SM
MD
LG