Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 16:55

Upinzani Uganda wasikitishwa na hatua ya serikali kufunga afisi ya haki za binadamu


Bobi Wine, Mwanasiasa wa upinzani nchini Uganda Uganda.
Bobi Wine, Mwanasiasa wa upinzani nchini Uganda Uganda.

Hatua ya serikali ya Uganda ya kufunga afisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za binadamu nchini humo, imezua shutuma kali kutoka kwa viongozi wa upinzani na wanaharakati, ambao wanasema inashiris kuendelea kuzorota kwa rekodi ya uhuru wa raia nchini humo.

Serikali ilimwambia Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Kibinadamu (OHCHR) wiki iliyopita, kwamba haitaongeza muda wa afisi yake katika nchi hiyo ya Afrika mashariki, hatua ambayo inamaanisha kwamba waangalizi wa haki za binadamu watafukuzwa.

Serikali ilisema katika barua kwa OHCHR mwezi huu kwamba uwepo wa Umoja wa Mataifa hauhitajiki tena ikidai imechukua hatua chanya katika kukuza uwezo wa ndani wa kufuatilia uzingatiaji wa haki za binadamu, ikiwa ni pamoja na kuibuka kwa jumuiya yenye nguvu ya kiraia.

"Utawala nchini Uganda unapaswa kutengwa na watu wote wanaotafuta demokrasia," Bobi Wine, nyota wa muziki aliyegeuka mwanasiasa, ambaye anaongoza chama cha upinzani cha National Unity Platform (NUP) alisema, akijibu swali kuhusu uamuzi wa serikali.

Naye Livingstone Sewanyana, ambaye anaongoza Wakfu wa Haki za Kibinadamu wa Uganda, hakukubaliana na sababu zilizotolewa na serikali za kufungwa kwa afisi hiyo. "Kwa miaka michache iliyopita...haki za raia zimekuwa zikiminywa," alisema.

Afisi hiyo ilianzishwa mwaka wa 2006 na imeangazia ukiukaji mkubwa wa haki ikiwa ni pamoja na kuteswa, kuwekwa kizuizini kinyume cha sheria, na serikali kukosa kuwashtaki watuhumiwa.

XS
SM
MD
LG