Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 14:10

Pande hasimu Yemen zakubali kubadilishana idadi kubwa ya wafungwa 


Watoto wanaoishi katika kambi za wakimbizi upande wa mkoa wa kaskazini wa al-Jawf nchini Yemen kutokana na vita kati ya majeshi ya serikali ya Yemen na wapiganaji wa kihouthi huko Marib, Yemen, Machi 8, 2020.
Watoto wanaoishi katika kambi za wakimbizi upande wa mkoa wa kaskazini wa al-Jawf nchini Yemen kutokana na vita kati ya majeshi ya serikali ya Yemen na wapiganaji wa kihouthi huko Marib, Yemen, Machi 8, 2020.

Pande hasimu zinazopigana vita nchini Yemen zimekubali kubadilishana wafungwa kiasi cha 1,000, wakiwemo raia 15 wa Saudi Arabia, Shirika la Habari la Uingereza Reuters limeripoti.

Hii ni moja ya hatua za kujenga uaminifu unaolenga azma ya kufufua mchakato wa mazungumzo ya amani yaliyokwama, Umoja wa Mataifa na vyanzo vingine vimesema Jumapili.

Serikali ya Yemen inayoungwa mkono na ushirika wa majeshi yanayoongozwa na Saudi Arabia, na harakati za Wahouthi wamekuwa wakipigana vita kwa zaidi ya miaka mitano.

FILE Vikosi vya Sudan vikiwa katika ushirikiano wa kijeshi unaoungwa mkono na Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu wakiondoa mabomu katika bandari ya Hodeidah, Yemen Jan. 22, 2019.
FILE Vikosi vya Sudan vikiwa katika ushirikiano wa kijeshi unaoungwa mkono na Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu wakiondoa mabomu katika bandari ya Hodeidah, Yemen Jan. 22, 2019.

Mwishoni mwa mwaka 2018 walisaini makubaliano ya kubadilishana takriban wafungwza 15,000 bainda ya pande zote lakini mkataba huo umekuwa ukitekelezwa polepole na ni baadhi tu ya vipengele vyake.

Pande hizo mbili hivi sasa zitawaachia huru watu waliokuwa wanazuiliwa na wafungwa 1,081, mwakilishi wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths amesema katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari wakiwa na Kamati ya Kimataifa ya Msalaba Mwekundu (ICRC).

Hatua hii inatekelezwa baada ya mkutano wa siku 10 wa kamati inayosimamia kubadilishana wafungwa uliofanyika katika Kijiji cha Uswizi cha Glion kilichopo Ziwa Geneva.

Viongozi wa pande zote mbili za kamati hiyo walikumbatiana baada ya kikao hicho, huku Griffiths akiwaambia : “Hongereni, hongereni.”

Vyanzo mbalimbali vyenye kufahamu mazungumzo hayo na Televisheni ya Masirah inayoendeshwa na Wahouthi wamesema kikundi hicho kitawaachia huru watu 400, wakiwemo raia wa Saudi Arabia 15 na wa Sudan wanne.

Wapiganaji wa Yemeni wanaounga mkono serikali ya nchi hiyo.
Wapiganaji wa Yemeni wanaounga mkono serikali ya nchi hiyo.

Nao ushirika wa majeshi unaongozwa na Saudi Arabia utawaachia wapiganaji wa Kihouthi 681 ikiwa idadi hiyo kubwa ya kubadilishana wafungwa tangu mazungumzo ya amani kuanza Stockholm Disemba 2018.

“Nazisihi pande zote zisonge mbele mara moja na kuwaachia huru wafungwa hao na kufanya kila juhudi kuendeleza hatua hii ili kwa haraka kukubaliana kuwaachia watu wengine zaidi wanaoshikiliwa,” Griffiths amesema.

Mkurugenzi wa ICRC wa Mashariki ya Kati Fabrizio Carboni, akiwa amekaa pembeni ya Griffiths, amezitaka pande mbili zinazopigana kutoa “uhakikisho wa usalama na takwimu” ili kurahisisha kuachiwa watu hao kwa haraka.

Timu za ICRC zitawahoji wale watakaoachiwa na kuwafanyia ukaguzi wa kiafya.

Yemen imegubikwa na vita tangu Wahouthi walivyoipindua serikali iliyokuwa inatambuliwa kimataifa katika mji mkuu, Sanaa, mwisho mwa mwaka 2014, na kupelekea ushirika unaoungwa mkono na nchi za Magharibi kuingilia kati mwezi Machi 2015.

Griffiths anajaribu kuanzisha tena mashauriano ya kisiasa kumaliza vita hivyo, ambavyo vimeuwa maelfu ya watu na kusababisha kile Umoja wa Mataifa ulichoelezea ni mgogoro mkubwa zaidi wa kibinadamu ambapo mamilioni wako hatarini kukabiliwa na njaa.


XS
SM
MD
LG