Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 01:58

Maporomoko ya ardhi yameua watu 109 nchini Rwanda na sita nchini Uganda


Mama akiwa amebeba mtoto akitoka katika nyumba iliyovamiwa na maji kutokana na mafuriko katika wilaya ya Rusizi
Mama akiwa amebeba mtoto akitoka katika nyumba iliyovamiwa na maji kutokana na mafuriko katika wilaya ya Rusizi

Watu 109 wamefariki kutokana na mafuriko na maporomoko ya ardhi magharibi na kaskazini mwa Rwanda.

Shirika la habari la serikali ya Rwanda- RBA, limeripoti kwamba waokoaji wanaendelea kuwasaidia manusura ambao wamekwama kwenye nyumbani zao.

Matope yameporomoka kutoka milimani na kufunga barabara, pamoja na kuharibu makazi ya watu

Gavana wa mkoa wa Magharibi Francois Habitegeko amesema kwamba maafisa wanafanya kila juhudi kufika katika kila nyumba iliyoharibiwa na kuhakikisha kwamba hakuna mtu aliyekwama kwenye nyumba hizo.

Watu 95 wamefariki katika mkoa wa magharibi.

Idadi ya vifo vya watu 109 inajumulisha watu waliofariki katika mkoa wa kaskazini.

Baadhi ya watu wameokolewa na kupelekwa hospitali. Maafisa hawajasema idadi ya watu waliolazwa hospitali.

Mvua kubwa zilianza kunyesha Jumanne saa kumi na mbili jioni kwa saa za Rwanda.

Watabiri wa hali ya hewa wametabiri kwamba mvua kubwa zitaendelea kunyesha mwezi huu wa Mei, katika nchi za Afrika mashariki.

Katika nchi Jirani ya Ugandaa, watu sita wamefariki kutokana na mafuriko katika wilaya ya Kisoro, kusini magharibi mwa nchi hiyo.

Kulingana na shirika la Msalaba Mwekundu, watu watano kutoka familia moja ni miongoni mwa waliofariki.

Mvua kubwa imekuwa ikinyesha nchini Uganda tangu mwishoni mwa mwezi Machi.

Maporomoko ya ardhi yameripotiwa katika baadhi ya sehemu za nchi hasa za milimani kama Kasese karibu na mlima Rwenzori ambapo nyumba kadhaa zimeharibiwa na mamia ya watu kukoseshwa makazi.

XS
SM
MD
LG