Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 06:30

Makamu wa Rais asema Magufuli anawasiliana na wananchi


Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan
Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema rais anawasiliana na wananchi na anaendelea kuwashauri waendelee kuchapa kazi.

‘’Mheshimiwa rais anawasalimia na anawashukuru sana sana, kwa kazi nzuri mlioifanya mwaka 2020 mwezi Oktoba ya kuirudisha serikali ya Chama Cha Mapinduzi madarakani, anasema tuko salama, tuchape kazi, tujenge upendo na mshikamano.’’ Samia Suluhu ameeleza.

Makamu wa Rais ameyasema hayo wakati wa kuanza ziara ya kikazi ya siku 5 Mkoani Tanga, akitembelea na kukagua Miradi ya Maendeleo ya Wananchi.

Samia pia amewaasa watanzania kuacha kusikiliza maneno ya watu wa nje na kuwa na umoja katika kipindi hiki.

‘’Nataka niwaambie katika wakati muhimu kwa watanzania kushikamana ni wakati huu, kujenga umoja ni wakati huu, si wakati wa kusikiliza maneno yanayotoka nje nasi yakatuparaganya vichwa, uimara wa taifa letu unaleta maneno mengi.’’ Samia suluhu amesisitiza.

Maelezo ya makamu wa rais yamekuja wakati kukiwa na uvumi katika mitandao ya kijamii kuhusu kutoonekana hadharani kwa Rais Magufuli na pia wasi wasi kuhusu afya yake.

Rais Magufuli alionekanaka hadharani mara ya mwisho Jumamosi, Februari 27.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alivunja ukimya, Ijumaa iliyopita na kuwahakikishia wananchi kuwa rais Magufuli anaendelea na shughuli zake, na sio lazima aonekane hadharani kila siku.

XS
SM
MD
LG