Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linatazamiwa kujadili Korea Kaskazini katika mkutano utakaofanyika Jumatatu kwa ombi la Marekani, kufuatia mfululizo wa majaribio ya makombora ya hivi punde zaidi mwaka huu.
"Hatua (za Korea Kaskazini) zinahitaji mshikamano wa pamoja na dhabiti wa jumuiya ya kimataifa," mawaziri wa Marekani, Japan, Kanada, Ujerumani, Uingereza, Ufaransa na Italia walisema.
Pyongyang ilifanya majaribio siku ya Ijumaa ya kombora la masafa marefu lenye uwezo wa kufika Marekani bara, muda mfupi baada ya kuonya kuhusu "majibu makali ya kijeshi" kwa Washington kuimarisha usalama wake katika eneo hilo.
Taarifa ya G7 ilisema jaribio la Ijumaa lilikuwa "kitendo cha kutojali" na "ukiukaji mwingine wa wazi" wa maazimio ya Umoja wa Mataifa.
"Msururu ambao haujawahi kushuhudiwa wa kurusha kombora la balestiki kinyume cha sheria uliofanywa na (Korea Kaskazini) mwaka 2022 ... ni tishio kubwa kwa amani na usalama wa kikanda na kimataifa," taarifa ya G7 ilisema.