Jeshi la Ethiopia lasisitiza mashambulizi ya anga Tigray yaliuwa waasi

Mkazi wa Togoga, aliyejeruhiwa kufuatia shambulizi la anga lililofanywa na Jeshi la Ethiopia huko Mekele akiepelekwa hospitali, Mekele mji mkuu wa Mkoa wa Tigray, Ethiopia, Juni 23, 2021.(Photo by Yasuyoshi CHIBA / AFP)

Msemaji wa jeshi la Ethiopia Alhamisi amesema mashambulizi ya anga yaliofanywa na jeshi mapema wiki hii katika jimbo la Tigray, yaliuwa wapiganaji na sio raia.

Kanali Getnet Adane ameliambia shirika la habari la Reuters katika mahojiano kwamba wapiganaji katika mji wa Togoga walikuwa wamevaa mavazi ya kiraia.

Jumanne, shambulizi la anga kwenye mji huo liliuwa watu 43, afisa wa matibabu ameiambia Reuters.

Shambulizi hilo lilifanyika baada ya wakazi kusema kwamba mapigano mapya yalipamba moto siku za karibuni kaskazini mwa mji mkuu wa Tigray, Mekelle.

Siku ya Jumatano mkazi wa mji huo aliiambia Reuters shambulizi la anga siku moja kabla liliharibu soko katika mji wa magharibi mwa Mekele. Mkazi huyo ameongeza kuwa binti yake wa miaka miwili alijeruhiwa katika shambulizi hilo.

Msemaji wa jeshi amesema wapiganaji hawakua ndani ya soko, lakini walikua wamekusanyika katika mji huo kuadhimisha kumbukumbu ya shambulizi la bomu katika mji mwengine katika jimbo la Tigray, ambalo lilifanyika mwaka wa 1988.

Chanzo cha Habari : Reuters na VOA News