Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 22:52

Zimbambwe : Wasifu wa marehemu Robert Mugabe


Marehemu Robert Mugabe
Marehemu Robert Mugabe

Robert Mugabe Rais wa kwanza wa Zimbabwe anaacha nyuma hiba ya uongozi wake wa miaka 37 katika taifa hilo la kusini mwa Afrika.

Kuna baadhi wanampongeza kwa kuwa shujaa wa ukombozi na wengine walikuwa wakimshutumu kwa kuharibu uchumi wa taifa ambalo liliwahi kuwa linajitosheleza kwa chakula katika bara la Afrika.

Mwaka 2017 naibu wake wa muda mrefu, Emmerson Mnangagwa alimlazimisha kujiuzulu na kuchukua wadhifa huo wa urais.

Mwaka 2018, kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miongo kadhaa, mamilioni ya Wazimbabwe walipiga kura zao katika uchaguzi ambao Mugabe hakuwemo kwenye karatasi ya kura.

Mugabe katika uchaguzi huo alikuwa miongoni mwa wapiga kura. Lakini itakumbukwa kuwa alikuwa kiongozi mwenye maneno makali na hakukubali kustaafu kimya kimya.

Alikuwa akitetea utendaji wake alipokuwa kiongozi wa taifa hilo la kusini mwa Afrika.

Marehemu Robert Mugabe, rais wa zamani wa Zimbabwe alieleza: "Enzi hizo nilikuwa muda wote nikipigania turejeshwe kwenye utaratiba wa kikatiba, kurejeshwa kwenye sheria, kurejeshwa kwenye uhuru kwa ajili ya watu wentu, kwenye mazingira ambayo watu wetu wanaweza kuwa huru."

Wazimbabwe wengi wengi wao wamezaliwa baada ya uhuru wa taifa hilo mwaka 1980, wanasema kuna ukweli katika hayo maneno.

Alikuwa shujaa, mpiganaji ambaye alifanya kila awezalo kudai uhuru wa Zimbabwe kutoka kwa waingereza mwaka 1979. Mwanzoni kabisa, aliwasihi Wazimbabwe kufikia maridhiano baada ya miaka 15 ya vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo vilipelekea kupatikana kwa uhuru wa taifa hilo.

Pia awali alipanua mifumo ya elimu na afya, na kuifanya nchi hiyo kuwa miongoni mwa zile zinazopigiwa mfano barani Afrika.

Uchumi wa nchi ulianguka baada ya kupitishwa kwa program mpya ya umiliki wa ardhi, na hivyo kusababisha kupanda kwa mfumuko wa bei na viwango vya juu mno vya ukosefu wa ajira.

Lakini hata wakati alipokuwa akipiga kura yake mwaka 2018, alifurahiwa sana na watu wake, ambao walimshangilia na kumuita kuwa ni mzee wa ukoo yaani GUSHUNGO.

Mugabe atazikwa katika makaburi ya mashujaa mjini Harare. Mugabe atakumbukwa na wazimbabwe na pia waafrika kwingineko barani humo.

Mungu ailaze roho yake mahali panapostahili.

Imetayarishwa na mwandishi wetu, Khadija Riyami, Washington, DC.

XS
SM
MD
LG