Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 07:34

Wananchi wa Qatar wasema wamefarijika kufunguliwa mpaka


Wasafiri kutoka Qatar wanaonyesha passport zao kwa maafisa wa uhamiaji wa Saudi Arabia wakiwa mpakani Salwa kuvuka kwenda Saudi Arabia Jan. 10, 2021.
Wasafiri kutoka Qatar wanaonyesha passport zao kwa maafisa wa uhamiaji wa Saudi Arabia wakiwa mpakani Salwa kuvuka kwenda Saudi Arabia Jan. 10, 2021.

Wananchi wa Qatar wamesheherekea kuvuka mpaka na kuingia Saudi Arabia Jumapili, wakiuita Ufalme huo ni “nchi yetu ya pili”, wakati Doha ikijitayarisha kuchukua hatua kali kudhibiti virusi vya corona kwa wananchi wa Saudi Arabia wanaoingia baada ya mvutano wa kidiplomasia wa nchi za Ghuba kumalizika.

Madereva waliwasili katika kivuko cha Salwa nchini Saudi Arabia, kilomita 500 mashariki mwa mji mkuu Riyadh, kutoka katik kivuko cha ardhini nchini Qatar kwenye eneo la Abu Samrah kwa siku ya pili baada ya kufunguliwa tena mpaka huo, waandishi wa AFP wanaripoti.

Saudi Arabia ilifunga upande wa mpaka na Qatar wa ardhini mwezi Juni 2017 ikiwa ni sehemu ya vikwazo ilivyo viweka ikidai ni majibu kwa Doha kuunga mkono vikundi vya Kiislam vyenye msimamo mkali na ushirikiano wake na Iran, limeripoti shirika la habari la AFP.

Qatar siku zote imekanusha madai hayo.

Saudi Arabia, pamoja na Umoja wa Falme za Kiarabu, Bahrain na Misri, zote kwa pamoja pia ziliiwekea Qatar marufuku ya kusafiri na biashara, wamekubali kuondoa vikwazo hivyo katika Mkutano wa Baraza la Ushirikiano la Ghuba uliofanyika Saudi Arabia Jumanne.

Qatar
Qatar

“Kuingia kwetu Saudi Arabia kutoka Qatar ni kama vile kuja katika nchi yetu ya pili, ambapo hakuna tofauti kati yet una wao katika tamaduni zetu,” amesema Mohammed al-Marri, mwananchi wa Qatar aliyekuwa amewasili Saudi Arabia.

Tangu kufunguliwa tena kwa mpaka huo, magari 167 kutoka Qatari yaliingia Saudi Arabia, huku magari 35 yakirudi Qatar kutoka Saudi Arabia, amesema Ali Lablabi, meneja mkuu wa idara ya forodha Salwa.

“Furaha hii – hakuna anayeweza kuielezea,” amesema Ghaith al-Marri, mwananchi wa Qatar. “Kuna watu ambao walianza kulia” wakati mpaka ulipofunguliwa tena, amesema.

Mashirika ya Ndege ya Qatar na Saudi Arabia yametangaza Jumamosi kupitia ujumbe wa Twitter kuwa wataanza safari zao kati ya nchi zao kuanzia Jumatatu.

Qatar imetangaza hatua kali za kudhibiti virusi vya corona kwa wale wanaowasili kutoka Saudi Arabia.

Doha itawataka wasafiri kuonyesha uthibitisho wa vipimo hasi vya virusi vya corona, na kufanyiwa vipimo tena mpakani na kuwekwa karantini katika hoteli iliyochaguliwa na serikali kwa wiki moja.

XS
SM
MD
LG