Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 18:48

Viongozi wa Afrika waendelea kutuma salamu za rambirambi kwa familia ya Malkia Elizabeth II


Malkia Elizabeth II alipokutana na Rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela.
Malkia Elizabeth II alipokutana na Rais wa zamani wa Afrika Kusini Nelson Mandela.

Salamu za rambirambi zinaendelea kumiminika kutoka Afrika  kufuatia kifo cha Malkia Elizabeth II, ambako malkia alikuwa alifanya ziara nyingi wakati wa utawala wake wa miaka 70.

Elizabeth alitawazwa kuwa malkia wakati akiwa nchini Kenya mwaka 1952, ziara yake ya kwanza nje ya nchi kama malkia ilikuwa Afrika Kusini. Baadaye alisaidia kuiongoza Uingereza katika kuhitimisha utawala wake wa kikoloni barani Afrika, wakati akihamasisha uhusiano mzuri na nchi mpya katika bara hilo.

Marais wa Ghana, Kenya, Nigeria na Afrika Kusini ni kati ya viongozi wa Afrika waliotuma ujumbe wa maombolezo kufuatia kufariki kwa Malkia wa Uingereza Elizabeth, ambaye alifariki siku ya Alhamisi akiwa na umri wa miaka 96.

Miaka ya awali ya utawala wa Malkia ilishuhudia kupoteza himaya yake ya koloni huko Afrika.

Uingereza wakati fulani ilikuwa inazitawala takriban nchi 17 za Afrika, na utawala wa waingereza bado unahusishwa na migogoro, kuchukua kwa nguvu rasilimali asilia na unyakuzi wa ardhi.

Ikemesit Effiong, mchambuzi wa siasa za kikanda aliyeko Lagos, Nigeria, alisema malkia alirekebisha mahusiano ya nchi yake baada ya kumalizika kwa utawala wa ukoloni katika nchi nyingi za Afrika.

“Na hasa, Uingereza imejenga na kuendeleza mahusiano mapana ya kiuchumi, kisiasa na utamaduni na nchi nyingi za bara la Afrika. Licha ya kuwepo hisia mseto zaidi katika misimamo ya muelekeo wa serikali za nchi nyingi za Kiafrika na Waafrika wengi kwa bara la Ulaya kwa jumla tangu kuanza kwa karne ya 21, mahusiano hayo mengi ya muda mrefu bado yanaendelea,” Effiong alisema.

Kenya ni moja ya nchi hizo ambazo Uingereza ilizitawala, na baadae Malkia Elizabeth alitangazwa malkia alipokuwa katika ziara nchini Kenya mwaka 1952, baba yake alipokufa wakati akiwa safarini.

Macharia Munene, mhadhiri wa mahusiano ya kimataifa katika Chuo Kikuu cha Marekani cha Afrika nchini Kenya, alisema kutawazwa kwa malkia kulisaidia kuharakisha nchi hii kujitawala.

“Huo ulikuwa wakati wa vuguvugu la kisiasa nchini Kenya,” alisema. “Kikundi cha Mau Mau kilikuwa kinakaribia kuanzisha mapigano na wapiganaji wake walikuwa wanafuatilia matukio ya Uingereza na hizo ndio hisia zilizojitokeza wakati vita vilipoanza. Walichoma miti, walijibu mashambulizi ya Waingereza na wakati akivishwa taji, [Wakenya] walimvika taji msichana wao na kumwita Malkia wa Mau Mau.

Effiong alisema Malkia Elizabeth alichukua msimamo tofauti na ule wa viongozi wa Uingereza waliomtangulia katika mahusiano yake na Afrika.

“Malkia Elizabeth alikuwa tofauti sana kwani alikuwa ni mtawala wa kwanza wa kifalme wa Uingereza kwa takriban karne mbili aliyewakilisha kusitisha ukoloni,” alisema, akiongezea kuwa aliwekeza katika uhalali wa ufalme, kama vile katika nchi za Jumuiya ya Madola yenye mahusiano na taasisi za kitamaduni.

Jumuiya ya Madola yenye mataifa wanachama 56, wengi wao lakini siyo yote yaliwahi kuwa chini ya utawala wa kikoloni wa Uingereza. Nchi wanachama wanakutana kuimarisha mahusiano yao na kutatua matatizo ya kimataifa pamoja.

Malkia alitembelea zaidi ya nchi 20 za Afrika wakati wa utawala wake, alianzia Afrika Kusini.

Munene alisema malkia alihakikisha anabadilisha taswira ya utawala wa kingereza.

XS
SM
MD
LG