Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 14:06

Trump na Biden wazuru Kenosha kitovu kipya cha mzozo wa ubaguzi Marekani


Makamu wa Rais wa Marekani Joe Biden, Kushoto. Rais wa Marekani Donald Trump.
Makamu wa Rais wa Marekani Joe Biden, Kushoto. Rais wa Marekani Donald Trump.

Wakati Mgombea kiti cha urais wa chama cha Demokratik Joe Biden akitembelea familia ya Mmarekani Mweusi aliyepigwa risasi na polisi mjini Kenosha, Rais Trump ametembelea jimbo la ushindani mkuu la Pennsylvania, Ikiwa imebaki miezi miwili kabla ya uchaguzi mkuu hapa Marekani.

Ziara ya Biden Alhamisi huko Kenosha ndio ya kwanza kuu nje, akianza kampeni yake baada ya kufanya kampeni kutokea nyumbani tangu mwezi June kutokana na janga la Corona na kutangaza mipango ya kutembelea majimbo mengine wiki ijayo.

Joe Biden Makamu Rais wa zamani alitembelea familia ya Jacob Blake Mmarekani Mweusi aliyepigwa risasi saba na polisi na amepooza sehemu ya chini ya mwili wake na kuhudhuria ibada maalum kwa niaba yake kwenye Kanisa la Grace Lutheran.

Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden akiongea na waumini wa Kanisa la Grace Lutheran Kenosha, Wis., Alhamisi Sept. 3, 2020. (AP Photo/Carolyn Kaster)
Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden akiongea na waumini wa Kanisa la Grace Lutheran Kenosha, Wis., Alhamisi Sept. 3, 2020. (AP Photo/Carolyn Kaster)

Akizungumza na baadhi ya wakazi amesisitiza juu ya mipango yake ya uchumi, elimu na kukarabati miji ili kupunguza ubaguzi na ukosefu wa usawa.

Alitembelea mji huo siku mbili baada ya Rais Trump kuutembelea mji huo wa Kenosha na kulaani kile alichokieleza ni ukiukaji wa sheria na ghasia zilizozuka huko.

Biden amesema : “Mimi ninafikiri tumefika kilele cha tatizo hili la ubaguzi katika historia ya Marekani. Ninaamini kwa dhati kwamba tuna nafasi nzuri sasa ya kuleta mabadiliko.

Kenosha ndio imekuwa kitovu kipya cha ugomvi wa ubaguzi wa rangi hapa Marekani baada ya Blake kushambuliwa na polisi wiki iliyopita.

Akiwa huko Biden alizungumza na baba yake Blake na familia yake na baadae kusema alizungumza na Blake mwenyewe kwa simu.

Trump kwa upande wake alipoutembelea mji huo alikutana na wafanyabiashara ambao maduka yao yalichomwa moto wakati wa maandamano na pia kuongea na maafisa wa polisi.

Rais Donald Trump akikagua uharibifu wa mali Kenosha, Wisconsin kufuatia ghasia zilizosababishwa na Jacob Blake kupigwa risasi na polisi.
Rais Donald Trump akikagua uharibifu wa mali Kenosha, Wisconsin kufuatia ghasia zilizosababishwa na Jacob Blake kupigwa risasi na polisi.

Biden vle vile alikutana na viongozi wa mji na maafisa wa polisi na kusisitiza kwamba ataongeza msaada kwa jamii ya walio wachache na kulaani ghasia wakati wa maandamano.

Biden alisema : Haijalishi ni kwa namna gani umekasirishwa, ikiwa unafanya wizi wa ngawira na kutia moto ni lazima uwajibishwe. Jambo hilo hatutalistahmilia.

Wakati wa ziara hiyo kampeni ya Biden ilitangaza ziara yake ya wiki ijayo katika majimbo ya Michigan na Pennsylvania ambayo ni muhimu kushinda kwani ndio majimbo yaliyompatia ushindi Rais Trump katika uchaguzi wa mwaka 2016.

Trump naye alirudi tena Pennsylvania Alhamisi na baada ya kutembelea majimbo mengine ya kati ya Marekani yanayofahamika kuwa na ushindani mkubwa.

Wachambuzi wanasema ingawa Biden anaongoza kwa ujumla kote nchini lakini wanahofia kwamba ujumbe wa Trump wa kuunga mkono polisi na sheria unapata nguvu katika majimbo hayo ya kati.

Karlyn Bowman wa taasisi ya American Enterprise hana mambo mengi ya kujivunia.

Bowman, ambaye pia ni mchambuzi wa kisiasa katika taasisi ya American Enterprise anasema : “Cha ajabu ni kwamba anaongoza katika uchunguzi wa maoni kuhusu masuala mawili tu, namna ya kushughulikia uchumi jambo ambalo amekuwa akiongoza. Lakini uchunguzi wa hivi karibuni kuhusu uhalifu mnamo wiki tatu zilizopita unaonesha Trump anaongoza.

Ingawa Biden anaongoza kitaifa mbele ya Trump lakini wachambuzi wanasema uchaguzi wa mwaka huu utakuwa ni mgumu sana kutabiri kutokana na hali ya kipekee ya mambo mwaka huu.

Imetayarishwa na mwandishi ketu, Abdushakur Aboud, Washington, DC.

XS
SM
MD
LG