Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 20:52

Trump na Biden warushiana maneno juu ya kukabiliana na ubaguzi


Rais wa Marekani Donald Trump, kulia na Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden.
Rais wa Marekani Donald Trump, kulia na Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden.

Kampeni za uchaguzi wa Novemba 3, 2020 hapa Marekani zimepamba moto wiki hii kati ya mgombea kiti cha rais wa chama cha Demokratik Joe Biden na mpinzani wake Rais Donald Trump mgombea wa chama cha Republican.

Wagombea hao wanarushiana maneno makali juu ya namna ya kukabiliana na ubaguzi wa rangi, maandamano na ghasia katika miji mbali mbali, na uhalifu unaoongezeka kote nchini.

Trump na Biden wameanza kampeni kabambe kwa kutembelea miji yenye kukumbwa na maandamano na ghasia hasa kufuatia tukio la mwisho la kupigwa kwa risasi na polisi, Mmarekani Mweusi, Jacob Blake karibu siku 10 zilizopita katika mji wa Kenosha na kusababisha maandamano na uharibifu wa mali katika mji huo.

Akitembelea huko Jumanne Trump alipita kwenye mtaa ambao maduka ya biashara yalitiwa moto na kukutana na maafisa wa usalama bila ya kukutana na familia ya Blake wala wakuu wa mji ambao ni wa demokrat.

Rais Donald Trump akiongea wakati anakagua uharibifu uliotokea kutokana na maandamano ya hivi karibuni dhidi ya ukatili wa polisi na kukosekana haki kwa watu wa rangi baada ya kupigwa risasi Jacob Blake na polisi wa Kenosha, Wisconsin, Marekani.
Rais Donald Trump akiongea wakati anakagua uharibifu uliotokea kutokana na maandamano ya hivi karibuni dhidi ya ukatili wa polisi na kukosekana haki kwa watu wa rangi baada ya kupigwa risasi Jacob Blake na polisi wa Kenosha, Wisconsin, Marekani.


Trump anawalaumu wa democrats kwa kuwezesha ghasia hizi anazozieleza ni ugaidi wa ndani.

“Ili kusitisha ghasia za kisiasa ni lazima pia kukabiliana na itikadi kali ambazo ni pamoja na ghasia hizi. Wanasiasa wa mrengo mkali wa kushoto wanaendelea kueneza ujumbe mbaya kwamba taifa letu na vikosi vyetu vya usalama ni wakandamizaji au wabaguzi. Ni lazima kuwapa msaada mkubwa walinda usalama wetu.”

Akiwa huko Kenosha Trump alipokelewa na wanaomuunga mkono na wanaompinga. Huku Familia ya Blake ikianda mkusanyiko wa amani wakitoa wito kukomeshwa ukandamizaji wa polisi dhidi ya wamarekani weusi na haki kutendewa kijana wao.

Biden kwa upande wake mapema wiki hii alitoa hotuba kali akimkosoa Trump, akisema ameshindwa kukabiliana na masuala mbali mbali ya nchi ikiwa ni pamoja na janga la Covid-19, uchumi wa nchi na anachochea ghasia badala ya kuzima.

“Rais aliye madarakani hawezi kusema ukweli , ameshindwa kukabiliana na ukweli na ameshinda kuunganisha taifa hili. Hataki kumulika taa ya ukweli bali anataka kuchochea ghasia katika miji yetu.”

Biden amelaani ghasia zinazofanywa na wafuasi wa itikadi kali za mrengo wa kushoto na kulia wakai Trump anakosoa wale wa mrengo kali wa kushoto bila ya kuwataja wale wa mrengo mkali wa kulia.

Namna rais anavyokabiliana na ghasia hizio zinazotokana na ubaguzi wa rangi ndio imekua suala kuu la uchaguzi kwa hivi sasa ambapo baadhi ya utafiti ukidokeza kwamba huwenda ikawahamasisha wamaekani weusi kujitokeza kwa wingi kupiga kura.

Lakini wachambuzi wengi wanadhani wamarekani wameshaamua ni nani watampigia kura.

Omar Wasow profesa wa sayansi ya siasa katika chou kikuu cha Princeton, anasema masuala haya huwenda hayatabadilisha maoni ya wapiga kura kwa hivi sasa.

“Uungaji mkono , hasa miongoni mwa wazungu , kwa vuguvgu la malalamiko umepungua kwa kiasi fulani. Lakini katika nchi hii iliyogawika wafuasi sugu wa Trump wako pale pale , na wafuasi wa biden wako wima nyuma yake, na hivyo hatushuhudi mabadiliko makubwa ya maoni licha ya matukio haya yote.”

Kilichobaki hivi sasa wachambuzi wanasema ni kwa Trump na Biden kuwahamasisha wafuasi wao katika miji ya mashambani kwenye majimbo yenye ushindani mkali kama huko Wisconsin. Biden hadi hivi sasa anaongoza katika uchunguzi wa maoni.


XS
SM
MD
LG