Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 05:33

Tanzania : Upelelezi kesi ya Barrick unaendelea, Mwanyika, Lugendo warudishwa rumande


Aliyekuwa Makamu wa Rais wa Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Acacia, Deo Mwanyika na Alex Lugendo wamefikishwa mahakamani.
Aliyekuwa Makamu wa Rais wa Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Acacia, Deo Mwanyika na Alex Lugendo wamefikishwa mahakamani.

Waendesha mashtaka katika kesi inayomkabili aliyekuwa Rais wa Migodi ya Pangea, North Mara, Exploration na Bulyanhulu, Deogratius Mwanyika na wenzake, wamedai mahakamani upelelezi bado ungali unaendelea chini ya usaidizi wa nje ya nchi.

Washtakiwa wanadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Aprili 11, 2008 na Juni 30,2007, katika sehemu tofauti za Jiji la Dar es Salaam, na mikoa ya Kahama, Shinyanga, Tarime (Mara) na (Biharamulo) Kagera maeneo ambayo yako katika Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Maeneo mengine ambayo washtakiwa wanadaiwa kutenda makosa hayo ni katika mji wa Johannesburg, Afrika Kusini, Toronto (Canada) na Uingereza.

Aidha, Mwanyika na Lugendo wanadaiwa kutoa msaada katika kusimamia mkakati wa kihalifu kwa nia ya kupata faida.

Washtakiwa hao wanadaiwa kutoa tamko la uongo kwa Kamishna Mkuu wa TRA huko Biharamulo kwa nia ya kukwepa kulipa kodi Dola za Marekani, 9,309,600 ambayo ilipaswa kulipwa TRA.

Mwanyika na wenzake wanakabiliwa na mashtaka 39, ikiwemo madai ya kutakatisha fedha na kukwepa kodi ya zaidi ya Dola za Marekani milioni 112, gazeti la Nipashe limeripoti nchini Tanzania.

Katika shtaka la kutoa nyaraka ya uongo, Mwanyika anadaiwa kuwa Aprili 30, mwaka 2018, katika Benki Kuu ya Tanzania, Ilala jijini Dar es Salaam, inadaiwa kwa makusudi aliwasilisha nyaraka ya uongo ya mkopo baina ya kampuni mgodi wa Bulyanhulu na Barrick International Bank Corp kwa madhumuni ya kuonyesha kuwa, kati ya Juni 2001 na Desemba 13, 2007 Bulyanhulu walijipatia mkopo usio na faida wa Dola za Marekani, 416,100,000 kutoka Barrick.

Maelezo hayo yalitolewa Ijumaa na Wakili wa Serikali, Simon Wankyo, mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Kevini Mhina.

Washtakiwa wengine katika kesi hii ni Meneja Uhusiano wa Mgodi wa Bulyanhulu, Alex Lugendo;Mkurugenzi Mtendaji wa Pangea, North Mara na Bulyanhuku, Assa Mwaipopo, kampuni ya Mgodi ya Pangea, North Mara, Exploration na Bulyanhulu.

Washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Oktoba 17, mwaka 2018.

"Mheshimiwa Hakimu upelelezi wa kesi hii bado unaendelea chini ya usaidizi wa nje ya nchi. Tunaomba tarehe nyingine ya kutajwa," alieleza Wankyo.

Hakimu alisema kesi hiyo itatajwa Aprili 12, mwaka 2019, na washtakiwa wataendelea kukaa mahabusu.

Katika kesi ya msingi, washtakiwa kundi la pili wanakabiliwa na mashtaka matatu ya kula njama, mashtaka saba ya kughushi, mashtaka 17 ya utakatishaji wa fedha, kuwasilisha nyarakaza uongokwaMamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) shtaka moja, kuongoza uhalifu wa kupangwa shtaka moja, mashtaka manane ya kukwepa kodi na moja la kutoa rushwa.

Pia Mwanyika na Lugendo wanadaiwa kuwa kati ya Desemba, 2009 na Desemba 31, mwaka 2018, katika maeneo tofauti ndani na nje ya nchi ya Tanzania, kwa pamoja na wengine ambao hawapo mahakamani, walisaidia mgodi wa North Mara kuhamisha Dola za Marekani, 374,243,943,45, huku wakijua kuwa fedha hizo ni zao la makosa ya kughushi na kukwepa kodi.

Aidha washtakiwa hao wanadaiwa kati ya Novemba 2, 2012 na Novemba 27, 2015 huko Shinyanga walitoa rushwa ya Sh. 718,520,001.76 kwa Hussein Kashindye ambayeni Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Mkoa (RCO) wa Shinyanga kwa lengo la kumshawishi ili aachane na uchunguzi wa makosa ya jinai yaliyokuwa yametendwa na mgodi wa Bulyanhulu.

Katika shtaka la kughushi, washtakiwa hao wakiwa na nia ya ulaghai, wanadaiwa walighushi mkataba wa mkopo wakitaka kuonyesha kwamba Aprili 30, 2014 Kampuni ya Pangea Limited ilikubali kukopa USD 90,000,000 ikiwa na riba kutoka benki ya kimataifa ya Barrick, huku wakijua kuwa si kweli.

Imetayarishwa na mwandishi wetu, Washington, DC

XS
SM
MD
LG