Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 13:38

Wawekezaji Tanzania washtushwa na hatua ya Magufuli


Rais Dr John Magufuli na Mwenyekiti wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation Prof John L. Thornton.
Rais Dr John Magufuli na Mwenyekiti wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation Prof John L. Thornton.

Miswada mitatu itayokayo walazimisha makampuni yanayochimba madini na nishati nchini Tanzania kurekebisha mikataba yao ni hatua ambayo imewashtua wawekezaji wa kigeni.

Miswada mitatu

Miswada mitatu iliwasilishwa na serikali ya Tanzania kwenye Bunge Alhamisi ambayo itairuhusu kuyalazimisha makampuni yanayochimba madini na nishati kufanya mazungumzo juu ya kurekebisha mikataba yao.

Shirika la Habari la Reuters limeripoti kuwa haikufahamika mara moja ni jinsi gani pendekezo la mazungumzo hayo juu ya mikataba litaathiri mradi wa Dola za Marekani bilioni 30 wa gesi, au sekta ya madini iliyoko tayari mashakani, ambayo inaiingizia Tanzania pato la asilimia 3.5 la uchumi wake wa ndani.

Malalamiko ya wafanyabiashara

Wafanyabiashara wamelalamika kuwa wanahisi Rais John Magufuli anawabana pasipo na haki kupitia tafsiri kadamizi za sheria za kodi, ikiwemo ongezeko la faini na madai ambayo wamekuwa wakiyaorodhesha kwa haraka katika soko la hisa la ndani ya nchi.

Lakini Magufuli anasema mageuzi hayo yataongeza uwazi na pato la taifa na kuwa makampuni yamekuwa hayalipi kodi stahili, madai ambayo wao wanayakanusha.

Miswada hiyo inategemewa kufanyiwa kazi haraka na bunge, na itawaathiri makampuni ya kimataifa na itafuatiwa na mapendekezo ya kamati inayofanya uchunguzi wa biashara ya machimbo ya dhahabu inayoendelea katika nchi hii ya Afrika Mashariki.

Marekebisho ya Sheria

Kamati hiyo imezitaka kufanyiwa mabadiliko ya haraka sheria zinazosimamia shughuli za uchimbaji madini, gesi na kodi.

Miswada hiyo mitatu inahusisha mikataba ya rasilmali asilia, mamlaka ya nchi kuhusiana na umiliki wa maliasili na marekebisho ya sheria zilizopo na kuiwezesha serikali kufanya mazungumzo tena au kusitisha mikataba.

Makampuni ambayo yataathirika ni pamoja na BG Group, ambayo ni sehemu ya Royal Dutch Shell, Exxon Mobil, Statoil na Ophir Energy.

Kampuni hizi zilikuwa na mpango wa kujenga kituo cha kusafirisha gesi nje (LNG) kitachogharimu dola bilioni 30, ikishirikiana na Kampuni ya taifa ya Tanzania Petroleum Development Corp.

Mswada wa utajiri asilia na rasilmali unasema: “Pale ambapo serikali imetoa taarifa ya kusudio la kuzungumzia tena utaratibu au makubaliano… na upande wa pili ukashindwa kukubaliana kujadiliana upya makubaliano ya masharti yasiokubalika au makubaliano hayakuweza kufikiwa… mahusiano yaliokuwepo yatasitishwa na kuchukuliwa kwamba yamefutwa.”

Inaeleza kuwa “masharti yasiyokubalika” ni kitu chochote ambacho ni “ kinyume cha maadili mazuri na utekelezaji wake unahatarisha maslahi ya watu” wa Tanzania.

Kikao cha Bunge

Hata hivyo kikao cha bunge kinachoendelea mjini Dodoma kimeongezewa muda wa siku kadhaa ilikuruhusu watunga sheria kupitia kwa makini miswada hiyo na kuipitisha, Spika wa Bunge la Taifa Job Ndugai amesema.

Tanzania ni nchi ya nne kwa uzalishaji mwingi wa dhahabu katika Afrika na imegundua maeneo makubwa yenye gesi lakini bado imebakia kuwa moja ya nchi maskini duniani.

Makampuni ya madini ambayo yanaweza kuathirika na mabadiliko ya sheria yaliyopendekezwa ni pamoja na AngloGold Ashanti, Acacia Mining Plc na Petra Diamonds.

Acacia ambayo inashughuli zaidi za uchimbaji Tanzania imekuwa ndio inayolengwa kutokana na Magufuli kukereka nayo.

Thamani ya hisa zake zimeporomoka nusu yake tangu Machi 3, wakati serikali ilipotoa katazo la kusafirisha madini kufuatia mgogoro wa kodi.

Acacia na AngloGold zimesema kuwa wamekuwa wakiipitia miswada hiyo. Mazungumzo kati ya Acacia na serikali kuhusu katazo la kusafirisha madini nje “bado hayajaanza.”

XS
SM
MD
LG