Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 18, 2024 Local time: 15:19

Somalia na Ethiopia kuiomba UN kuondoa marufuku ya silaha dhidi ya Mogadishu


Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamud (kushoto) akiwa na mwenyeji wake Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed.
Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamud (kushoto) akiwa na mwenyeji wake Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed.

Somalia na Ethiopia zinasema zitafanya kazi pamoja  kulinda maeneo ya pande zote mbili, ikiwemo kuliomba Baraza la Usalama la UN kuondoa marufuku ya muda mrefu ya silaha kwa  Mogadishu.

Katika mwisho wa ziara yake ya siku mbili mjini Addis Ababa, Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamud alisaini tamko lenye nukta kumi na mwenyeji wake, Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed.

Kuboresha na kuimarisha ushirikiano wa muda mrefu wa pande mbili na uhusiano kati ya nchi hizo mbili na watu wake ulijikita katika kuheshimu mipaka na uhuru wa nchi zote mbili,” tamko lao lilieleza.

Kipaumbele kitakuwa ni kutaka Somalia kupewa tena uwezo wake wa kununua silaha na kuimarisha ulinzi wa majeshi yake ya usalama.

“Viongozi wamelitaka Baraza la Usalama la UN kufikiria ombi hilo la serikali ya shirikisho ya Somalia kwa kuiondolea marufuku ya silaha iliyowekewa kwa zaidi miaka 30, ili kuhakikisha Somalia inajitosheleza kwa silaha ili iweze kikamilifu kukabiliana na vitisho vya usalama vinavyofanywa na kundi la kigaidi la Al-Shabaab,” taarifa hiyo ya viongozi hao iliongeza.

Somalia imepigwa marufuku kununua silaha yenyewe, marufuku ya zamani iliyowekwa mwanzoni mwa miaka ya 1990 ili kuwazuia wababe wa vita kuikamata nchi hiyo wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Lakini marufuku hiyo imeongezewa muda katika siku za nyuma, ikibadilika kuwalenga wapiganaji wa Al-Shabaab. Hivi leo, Somalia inaweza tu kununua aina fulani ya silaha, na kwa idhini kutoka kamati ya vikwazo ya UNSC.

Wafadhili na nchi nyingine zinazoisaidia Somalia kulijenga upya jeshi lake wanaweza kutoa msaada wa silaha tu, lakini lazima baraza hilo lijulishwe.

Wakosoaji wanasema kuwa hili linakinzana na haki ya Somalia kuimarisha majeshi yake ya usalama ikipelekea jeshi hilo kuwa na silaha duni ukilinganisha na wanamgambo wa Shabaab ambao wananunua silaha zenye nguvu zaidi katika soko la magendo.

Chanzo cha habari hii kinatokana na gazeti la "The East African" linalochapishwa nchini Kenya

XS
SM
MD
LG