Kutokana na kuchoshwa na kufungwa kwa shughuli za kawaida kufuatia janga la Corona, wamarekani wengi sasa wana ari ya kusafiri baada ya hali ya kawaida kurejea.
Inakadiriwa kwamba wamarekani takriban milioni 55 wamesafiri kwa kutumia barabara, ndege na treni, wakati safari za ndege zikisemekana kurejea kwa takriban asilimia 99 ikilinganishwa na mwaka 2019 wakati wa kipindi cha janga la Covid-19.
Hata hivyo uhaba wa wafanyakazi wa kutosha wa ndege pamoja na ndege zenyewe kumeathiri sekta hiyo, wakati idadi ya viti ikipungua pia, pamoja na kupanda kwa nauli za kusafiria.
“Msimu huu wa siku kuu unakisiwa kuwa wenye msongamano mkubwa sana katika historia ya Marekani, ukifuatia kwa karibu msimu wa joto ambao pia ulivunja rekodi” amesema waziri wa uchukuzi wa Marekani Pete Butiigieg.
Mkesha wa Thanksgiving Jumatano jioni kwa kawaida huwa wenye shuguli nyingi zaidi. Hata hivyo uwezo wa kufanya kazi kwa njia ya kimitandao umewawezesha wamarekani wengi kusafiri mapema kabla ya misongamano kuanza.
Shirika la ndege la United Airlines lilisema kwamba linatarajia kubeba abiria milioni 5.5 kuanzia Novemba 18 hadi 30 ikiwa idadi inayokaribia kipindi kilichotangulia ni janga la corona 2019, likiwa pia ongezeko la asilimia takriban 12 kulinganishwa na mwaka uliopita.
Inakisiwa kwamba Novemba 27 kuwa siku yenye wasafiri wengi zaidi tangu kipindi cha covid.
Upungufu wa safari za ndege pamoja na ongezeko la watu wanaotaka kusafiri vimepelekea bei za nauli kupanda. Nauli wakati huu wa Thanksgiving zimepanda kwa asilimia 17 kulinganishwa na mwaka jana pamoja na bei za mwaka 2019, kulingana na app ya safari za ndege ya Hopper. Nauli za kimataifa pia zinasemekana kupanda kwa asilimia 30 kulinganishwa na mwaka 2019.
"Iwapo ndege yako itaahirishwa au kuchelewa kwa sababu moja au nyingine, nataka umma ufahamu kwamba una haki ya kurejeshewa fedha zao iwapo utaamua kufuta safari yako. Iwapo utakumbana na tatizo pale kampuni ya ndege ikikataa kuheshimu makubaliano hayo, basi huna budi kutufahamisha” alisema Waziri huyo wa wa Uchukuzi.
Takwimu pia zimeonyesha kwamba kuna ongezeko kwenye mifumo mbadala ya usafiri kama vile mabasi na treni. Zaidi ya watu milioni 1.4 wameondoka kwenye miji yao wakati wa siku kuu ya Thanksgiving kwa kutumia basi au treni, idadi ambayo kwa ujumla inakadiriwa kufika wasafiri milioni 55.4 kote Marekani. Hilo ni ongezeko la kiasi fulani ikilinganishwa na mwaka jana kulingana na shirika la wamiliki wa magari hapa Marekani la AAA.
Afisa katika shirika la wamiliki wa magari hapa Marekani la AAA, Marie Montgomery amesema
“Tunashauri watu kujipa muda na pia wawe na subira hasa iwapo wanasafiri wakati siku kuu ikiwa imekaribia kama Jumanne na Jumatano pamoja na baada ya mwisho wa wiki pale wanaporejea mwakwao”.
Rais wa Marekani Joe Biden alisafiri Jumanne usiku kutoka kituo cha ndege cha kijeshi cha Andrews akielekea Nantucket Massachusetts akiandamana na mke wake Jill Biden ili kuungana na familia zao kwenye kisiwa hicho.
Hata hivyo wakati wa kuondoka Biden hakuzungumza na wanahabari kando na kuwapungia mkono kabla ya kuingia ndege.
Hapo Jumatatu batamzinga wawili wa Thanksgiving waliletwa kwenye Ikulu ya White House ikiwa sehemu ya utamaduni wa kila mwaka ambapo rais aliwaokoa kutokuwa kitoweo cha mtu wakati wa sherehe.
Forum