Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 00:05

Serikali yawapiga marufuku wachunguzi wa UN kuingia Burundi


Wachunguzi wa Tume ya Umoja wa Mataifa juu ya uvunjifu wa haki za binadamu wakitoa ripoti yao Septemba 5, 2018, huko Geneva. Kutoka kushoto ni Francoise Hampson wa Uingereza (kushoto, na Doudou Diene wa Senegal (kulia).
Wachunguzi wa Tume ya Umoja wa Mataifa juu ya uvunjifu wa haki za binadamu wakitoa ripoti yao Septemba 5, 2018, huko Geneva. Kutoka kushoto ni Francoise Hampson wa Uingereza (kushoto, na Doudou Diene wa Senegal (kulia).

Serikali ya Burundi imetangaza kwamba wachunguzi wa Umoja wa Mataifa walio chapisha hivi karibuni ripoti inayo wanyooshea vidole viongozi wa nchi hiyo, akiwemo Rais Pierre Nkurunziza, juu ya uchochezi wa uhalifu na vitendo vingine vya ukiukwaji wa haki za binadamu, wamepigwa marufuku kuingia Burundi.

Vyanzo vya habari nchini Burundi vinasema agizo hilo la serikali limetolewa Jumanne na Waziri wa Mambo ya Nje Ezechiel Nibigira, baada ya Bunge na Baraza la Seneti la Burundi kukutana katika kikao maalum jana na kuiomba serikali kuwafungulia mashtaka wachunguzi hao kwa kile wanachosema wamewazulia uongo viongozi wa nchi hiyo.

Wachunguzi hao waliopigwa marufuku kuingia Burundi ni Doudou Diene kutoka Senegal, Lucy Asuagbor kutoka Cameroon na Francoise Hampson kutoka Uingereza.

Wakati huo huo, Makamu Kamishna wa Baraza la Umoja wa Mataifa inayo simamia haki za binadamu, Kate Gilmore, katika kikao kuhusu hali ya uvunjifu wa haki za binadamu nchini Burundi, kilicho fanyika Jumanne, mjiini Geneva, amekiambia kikao hicho kwamba baraza hilo halitoweza kutoa ripoti kuhusu hali halisi ya haki za binadamu Burundi.

Kamishna amesema sababu iliyopelekea hilo ni kuwa serikali ya Burundi ilipinga kushirikiana na tume ya wataalamu wa UN wa masuala ya haki za binadamu, waliotumwa nchini Burundi, mwezi Machi, 2018, baada ya kuwepo makubaliano na serikali ya Burundi.

Lakini baadae serikali mwezi Aprili ikatangaza kusitishwa kwa vibali vyao vya kuwawezesha kuendelea na kazi yao nchini Burundi.

UN tayari ilitoa maazimio ambayo yalitakiwa kutekelezwa nchini Burundi, lakini serikali hiyo ilizuia utekelezaji wa maazimio hayo, amesema Gilmore.

Amesema sehemu ya maazimio hayo ilikuwa ni kufuatilia hali ya uvunjifu wa haki za binadamu unaofanywa na vyombo vya usalama nchini humo.

XS
SM
MD
LG